NA MWANDISHI WETU
MIGOGORO ya ardhi nchini ni sawa na mfupa mgumu. Hivi ndivyo unavyoweza kusema baada ya Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba, kuwaagiza Mwanasheria Mkuu wa serikali na mawaziri wawili kuja na mapendekezo yatakayotoa ufumbuzi wa migogoro hiyo.
Mawaziri waliopewa kibarua hicho ni wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWMñTAMISEMI).
Waziri Mkuu Dk. Mwigulu alilazimika kutoa maagizo hayo, akiwa katika Halmashauri ya Sumbawanga mkoani Rukwa ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa ziara yake, ambako alisikiliza na kukatua kero za wananchi.
“Wachambue tujue hasa tunaponasa ni wapi haiwezekani kila wilaya asilimia 99 ya migogoro ya ardhi na tukaacha suala hili liendelee kama ni muundo tunaofanyia haufanyi kazi tuufumue,”alisema.
Alisema kama itawezekana watoe mapendekezo ya muundo ambao utakwenda kutoa majawabu ya kudumu ya mambo hayo.
“Kwa mfano kuna maeneo mengine nimepita wilaya nyingi zina mahakama hazina mabaraza kwa hiyo tunamtoa mwananchi pale kwenye wilaya aende hadi mkoani kufuata baraza umbali huu unawanufaisha wale wanaowaonea walio maskini kwa kuwafuatilia hadi anakata tamaa,”alisema.
Dk.Mwigulu alisema migogoro ya ardhi imekuwa ni kichaka na kwamba wanajua kuwa watu wanaofuatilia masuala ya ardhi watachoka.
“Kila kona kumekuwa na migogoro ya ardhi tunataka kufanya kama migogoro hiyo ni sehemu ya maisha yetu sasa nimwelekeze Mwanasheria Mkuu wa serikali, Waziri wa Ardhi, Waziri wa Tamisemi waje na ufumbuzi ambao utatatua matatizo hayo ya muda mrefu,” alisema.
“Hatuwezi kuendelea na utaratibu huu watu wakishalitamani eneo wanamwangalia mmiliki wanampima hivi nauli yake anaweza kufuatilia miaka mingapi wanakwenda wanachukua,”alisema.
Alisema kuna maeneo mengine wanakuwa wanawahesabu idadi ya wajumbe wa Baraza la Ardhi na wanawawekea bajeti.
“Wanaweka bajeti wanajua bado bajeti hiyo ni ndogo kuliko eneo lenyewe kununua sasa hii lazima tuanze upya na lazima tumalize haya,”alisema.
Alisema amepita kila kona kumekuwa na migogoro ya ardhi.
Dk.Mwigulu amemtaka Mkuu wa mkoa wa Rukwa na watu wake wa ardhi kuanza kutatua migogoro hiyo kwa ngazi ya mkoa.
“Lakini kwa tiba ya kudumu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWMñTAMISEMI)ebu kaeni kwa dharura, wataalamu wenu mfanye tathmini kama ya kisera, kisheria, kimuundo lazima tupate majawabu,” alisema.
Alisema lazima machozi ya wananchi yafutwe ambapo kila kona wamekuwa wakilia kuhusu migogoro ya ardhi.
“Hii ni suala linalotishia undugu wetu kila eneo na bahati mbaya sana ardhi haiwezi kuongezeka sisi tunaongezeka, lakini ardhi haiwezi kuongezeka,” alisema.
Dk. Mwigulu aliwaahidi wananchi kuwa akipata taarifa kutoka kwa viongozi hao atakuja na utaratibu ambao atamshauri Rais Dk. Samia Suluhu Hassan aelekeze utekelezwe kwa ajili ya kukomesha jambo hilo.
Akitoa malalamiko yake kuhusu fidia ya ardhi iliyopo eneo la Katai Magereza, Subastia Ghabeir
alisema wilaya ya Sumbawanga ilitwaa eneo hilo na kujengwa nyumba saba huku wakidai kumfidia viwanja viwili.
“Nilipeleka karatasi ya malalamiko ya fidia ya ardhi yangu wakaniambia nisubiri wataniita alafu baadaye wakaniambia niweke alama ya kidole kwenye karatasi wakaniambia kesho watanipa fedha,”alisema.
Alisema kesho yake alipoenda akawaambia wampe fedha zake kwa ajili ya fidia ya ardhi yake lakini hawakumpatia.
“Mimi sitaki viwanja wanipatie fedha nitumie mimi sitaki hata hayo mashamba wanipe fedha kutokana na kuwa shamba langu ni kubwa nilikuwa nafuatilia kwa kutembea sasa ninashindwa kutembea ninatambaa,” alisema.
Alisema wanataka kumpatia ardhi ya nini wampatie fedha naomba Waziri Mkuu unione huruma.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halamshauri ya Sumbawanga, Pendo Mangali alisema anamwomba mhusika avumilie hadi mwisho wa mwezi huu watamlipa.
“Kwa sababu mwezi huu tunakusanya mapato na mapato yetu si makubwa sana ninaomba nikuhakikishie Waziri Mkuu nimeahidi mbele yako na mbele ya umati huu nitamlipa,” alisema.
Katika kutatua changamoto hiyo Waziri Mkuu Dk. Mwigulu alimtaka mhusika ataje gharama ya fidia ya ardhi yake na ndipo alipotaja kiasi cha sh. milioni 23.
Mnamo Januari 13 mwaka huu Rais Dk.Samia Suluhu Hassan, alisisitiza masuala ya migogoro ya ardhi inapaswa kushughulikiwa kupitia mahakama badala ya mabaraza ya ardhi, huku akieleza kuwa mfumo huo utaimarisha upatikanaji wa haki kwa wananchi na kuongeza ufanisi katika utoaji wa maamuzi.
Rai Dk.Samia alisema hayo wakati ufunguzi wa mkutano mkuu wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA), uliofanyika katika viunga vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania,jijini Dodoma.
Alisema Serikali inalenga kuhamishia usikilizwaji wa migogoro hiyo katika Mahakama za Mwanzo na kwamba hatua hiyo itahitaji uwekezaji mkubwa, ambapo Serikali imeanza maandalizi ya kutenga bajeti ya kutosha katika mwaka wa fedha ujao kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama za Mwanzo nchi nzima.
Kwa mujibu wa Rais Dk.Samia, maboresho hayo yataondoa ucheleweshaji wa mashauri ya ardhi, kuongeza uwazi katika maamuzi na kupunguza migogoro inayodumu kwa muda mrefu, hatua inayotarajiwa kuleta utulivu na amani katika jamii.




