Na NJUMAI NGOTA,
Iringa
MGOMBEA Mwenza wa Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, amesema Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amebainisha kwa vitendo mwanamke wa Kitanzania anapopewa fursa ya kuongoza anatekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa na kuleta matokeo makubwa ya maendeleo.
Balozi Dk. Nchimbi amesema hayo Isimani, alipohutubia mamia ya wananchi katika mkutano wa kampeni za Chama kuelekea uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 29, mwaka huu.
Amesema hofu ilikuwepo kipindi Rais Dk. Samia anaingia madarakani miaka minne na nusu iliyopita, hivi sasa imefutwa na matendo yake makubwa, ambayo yamejidhihirisha katika kila sekta ya maendeleo ya taifa.
“Rais wetu ametuongoza kwa ufanisi. Ametimiza kiapo chake cha kuimarisha mshikamano, kuendeleza umoja wa taifa letu, kulinda mipaka na uhuru wa taifa letu na ameweka historia ya pekee ya mafanikio katika nyanja zote,” amesema.
Mgombea Mwenza wa Urais amesema mfano wa Rais Dk. Samia umekuwa kielelezo hadi kwa mataifa mengine na hivi sasa yanauliza kiongozi wa aina yake watampata wapi.
“Amedhihirisha kwa vitendo kwamba, wanawake wa Kitanzania wakipewa fursa wanaweza. Leo Samia amekuwa kiongozi wa mfano ndiyo maana nchi nyingine zimekuwa zikihoji zitampata wapi kiongozi kama Samia, tunawaambia tafuteni wenu,”amesema.
Balozi Dk. Nchimbi ameeleza mikakati ya CCM kwa miaka mitano ijayo kupitia ilani yake ya mwaka 2025-2030 ikiwemo kujenga vituo vipya vya afya saba, zahanati 15 na kupandisha hadhi ya hospitali ya wilaya.
Kuhusu sekta ya elimu, amesema itapewa kipaumbele kwa kuongeza shule 12 za msingi, sekondari nane na madarasa 395 katika shule zilizopo.
Amesema mradi mkubwa wa maji utaanzishwa Isimani na utawanufaisha wananchi katika zaidi ya maeneo manane, sanjari na uchimbaji wa visima virefu vitano na kukamilisha miradi mingine minne.
Kwa upande wa kilimo, Dk. Nchimbi amesema wamekusudia kuongeza ruzuku ya mbolea, kuboresha skimu za umwagiliaji, kujenga mifereji mipya na ghala la kuhifadhi mazao ya parachichi.
Akizungumzia sekta ya ufugaji, Balozi Dk. Nchimbi alisema wataimarisha ruzuku ya dawa na chanjo, kujenga majosho, malambo na mabwawa ya samaki vijana wapate fursa za ajira na kipato.
Vilevile, alisema mazingira ya biashara yataboreshwa kwa wajasiriamali na barabara zaidi ya tano zitajengwa kwa kiwango cha lami na zaidi ya 10 kwa kiwango cha changarawe.
Balozi Dk. Nchimbi alimwombea kura Rais Dk. Samia, wabunge na madiwani, wahakikishe Oktoba 29, mwaka huu, wanakipigia kura Chama.
Kwa upande wake, Mgombea Ubunge wa Isimani, William Lukuvi, alimshukuru Dk. Samia kwa kumuona Balozi Dk. Nchimbi.
Lukuvi alisema rekodi ya uongozi wa Dk. Nchimbi serikalini na ndani ya CCM inajulikana wazi, kuanzia Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), mkuu wa wilaya, naibu waziri hadi waziri na mjumbe wa vikao vikuu vya chama.
Lukuvi alisema rekodi hiyo inawapa wananchi imani kuwa ndiye mtu sahihi wa kumsaidia Rais Dk. Samia katika safari ya kuendeleza taifa.
“Wananchi wa Isimani wanajua rekodi yako. Uadilifu wako, uzalendo wako na misimamo yako imara ndiyo sababu tunasema kwa dhati hatuna shaka na wewe. Hadi Oktoba 29 nitakuwa nikiwaambia wananchi wewe ni nani,”alisema.
Lukuvi aliwaomba wananchi wa Isimani Oktoba 29, mwaka huu, wajitokeze kwa wingi na kumpigia kura Dk. Samia katika urais, wabunge na madiwani wanaotokana na CCM.Awali, akiwahutubia mamia ya wananchi katika
Uwanja wa Mpira wa Isere, Jimbo la Kilolo, katika mkutano wa hadhara wa kampeni za Chama za kuomba kura kuelekea Uchaguzi Mkuu, Mgombea mwenza huyo, Dk. Nchimbi, aliainisha baadhi ya vipaumbele vitakavyotekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo, huku sekta ya kilimo, afya, elimu, miundombinu na nishati vikitajwa kama nguzo kuu za maendeleo ya wananchi wa eneo hilo.
Alisema vipaumbele hivyo vitatekelezwa kupitia Ilani ya Uchaguzi ya Chama ya mwaka 2025-2030, iwapo CCM itapewa ridhaa ya kuongoza nchi katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Alisema dhamira ya Dk. Samia ni kuendeleza jitihada za kuwaletea maendeleo wananchi kwa kasi zaidi katika miaka mitano ijayo.
Alibainisha kuwa,katika kipindi cha miaka mitano ijayo Chama kimekusudia kuboresha Hospitali ya Wilaya ya Kilolo kwa kuongeza majengo, vitendea kazi na rasilimali watu kwa lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi.
Pia, Balozi Nchimbi alisema wamedhamiria kujenga vituo vipya vya afya vitano na zahanati 10 kufanikisha upatikanaji wa huduma bora karibu na wananchi.




