Na MUSSA YUSUPH,
LINDI
MGOMBEA Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema serikali imepeleka umeme wa kutosha vijijini ambao utaweza kuhudumia kongani za viwanda.
Dk. Samia aliyasema hayo alipohutubia maelfu ya wananchi katika mkutano wa kampeni uliofanyika wilayani Ruangwa mkoani Lindi.
Alisema serikali imetanguliza nishati ya umeme ya kutosha kwa lengo la kuanzisha kongani za viwanda kwa sababu sekta ya hiyo inakuwa kwa kasi.
Dk. Samia alibainisha kuwa umeme huo utarahisisha maendeleo ya viwanda na kukuza uzalishaji.
Katika mkutano huo, Dk. Samia alieleza mkakati wa kudhibiti wanyamapori waharibifu wanaovamia mashamba ya wananchi.
Dk. Samia alisema serikali inafahamu mahitaji ya wananchi yanaongezeka, kwa sababu hiyo itaendelea kufanyia kazi sekta zote za maendeleo ya jamii ili wilaya hiyo ipige hatua zaidi.
“Vituo vya afya nane vipya vimejengwa, nikawa namuuliza Waziri Mkuu (Kassim Majaliwa) mnakata ngapi? Akaniambia zipo kata zaidi ya 20, nikaelewa kwamba kazi bado ipo.
“Bado tutakuja kujenga vituo vya afya, bado tutakuja kujenga zahanati, shule za msingi na sekondari. Tutahakikisha miradi yote ya maji inayotekelezwa inakamilika ili kila Mwanaruangwa apate maji safi na salama,” alibainisha.
Vilevile, alisema serikali inakwenda kukamilisha kuunganisha umeme katika vitongoji kuwezesha nishati hiyo ikatumike nyumbani, kulinda usalama na shughuli za uzalishaji.
“Niwaahidi kwamba kazi ipo na tunakuja kuifanya. Naelewa katika maeneo ya vijiji vya Madangilo, Magawa, Lugombe na Mbwemkulu kuna tatizo la wanyama kufanya uharibifu kwenye mashamba.
Alibainisha: “Hili ninalielewa vyema na mkiwakuta wale wanyama waambieni dawa yao ipo jikoni. Wanyama tunawapenda lakini lazima tuwalinde, tuwazuie wabaki kwenye hifadhi zao.”
Alisema hatua mbalimbali zinachukuliwa kuhakikisha wanyamapori hawaingii katika mashamba ya wananchi.




