Na NJUMAI NGOTA,
Pwani
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimesema Dk. Samia Suluhu Hassan, ameonesha kwa vitendo uwezo mkubwa wa usimamizi wa Ilani ya Chama, akijidhihirisha siyo mlalamikaji, bali kiongozi anayetoa majawabu ya matatizo ya Watanzania.
Kauli hiyo, imetolewa na Mgombea Mwenza wa Urais wa CCM, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, katika Jimbo la Rufiji, mkoani Pwani, alipohutubia mamia ya wananchi katika mkutano wa hadhara wa kampeni za Chama kuelekea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29, mwaka huu.
“Katika miaka minne na nusu iliyopita, hakuna kiongozi yeyote Afrika Mashariki na Kati, aliyevunja rekodi ya miradi inayogusa huduma za jamii zaidi ya Dk. Samia Suluhu Hassan.
“Mambo aliyoyafanya katika huduma za afya, elimu, miundombinu Afrika Mashariki hakuna anayemsogelea kwa miaka minne na nusu, huwezi kufanya mambo haya kama huguswi na maisha ya kawaida ya Mtanzania,”alisema.
Alisema Dk. Samia, amekuwa akiguswa na maisha ya kawaida ya Mtanzania, jambo ambalo, ndiyo msingi wa mafanikio ya serikali yake katika nyanja zote.
“Anateswa na umaskini wa watu wetu, kila sekta inayohusika na kubadilisha maisha ya Mtanzania, Dk. Samia kafanya kazi ambayo haina mfano wake,” alisema.
Dk. Nchimbi, alisema ndiyo maana wanaCCM wanapita kifua mbele nchi nzima, wakikinadi Chama na Dk. Samia bila aibu, kwa sababu aibu zetu ameziondoa.
MIAKA MITANO IJAYO RUFIJI
Alisema katika miaka mitano ijayo, iwapo watapewa ridhaa ya kuongoza nchi, baadhi ya vipaumbele vitakavyotekelezwa Wilaya ya Rufiji ni kujenga shule nne za msingi, zahanati tano, vituo vya afya vinne, nyumba saba za walimu na madarasa katika shule 2001 za msingi.
Kuhusu sekta ya kilimo, alisema wamedhamiria kuwaongezea shamba la mikorosho lenye ekari 2,000 kutoka 1,000, mifumo ya umwagiliaji inaboreshwa na ghala kubwa la kuhifadhi mazao, litajengwa kusaidia wakulima wa Rufiji kupata masoko na kuepuka hasara.
Pia, alisema kwa upande wa maji, miradi zaidi ya 15 itajengwa na kukarabatiwa yakiwemo ya maeneo ya Kikobo, Kishera, Mupi, Bwawani, King’ongo, Kipo, Mahoro Moro na Kilimani.
Kwa mujibu wa Dk. Nchimbi, miundombinu ya barabara na daraja, serikali imekusudia kukamilisha ujenzi wa barabara ya lami na kilometa katika mabano Utete–Nyamwage (33), Ikwiriri–Mkongo (30), barabara za Mji wa Utete (10), daraja la Mbambe na barabara unganishi (3), daraja la Muhoro (mita 80) na mifereji ya mvua (10).
Akiwa wilayani Kibiti, Dk. Nchimbi, alisema katika miaka mitano ijayo, wamepanga kuiimarisha hospitali ya wilaya, vituo vya afya vitatu vipya, zahanati sita mpya, shule za msingi na sekondari, soko na stendi mpya ya kisasa.
Dk. Nchimbi, alisema kilimo na ufugaji, serikali itaimarisha skimu za umwagiliaji, kujenga maghala ya kuhifadhi nafaka, mabwawa mapya ya kufugia samaki na minada ya mifugo.




