Na MWANDISHI WETU
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, leo Jumanne Novemba 18, 2025, kwa mamlaka aliyonayo, ameunda Tume huru ya kufanya uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea nchini kipindi cha Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, mwaka huu.
Katika taarifa ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dk. Moses Kusiluka, Mohamed Chande Othman, Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, ndiye aliyeteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Tume hiyo.
Wajumbe watakaofanya kazi na Jaji mstaafu Chande ni pamoja na Profesa Ibrahim Hamis Juma, Jaji Mkuu mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Balozi Ombeni Yohana Sefue, Mwanadiplomasia na Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu na Balozi Radhia Msuya, Mwanadiplomasia na Balozi Mstaafu.
Wengine ni Balozi Luteni Generali Paul Meela, Mwanadiplomasia na Balozi Mstaafu, Mkuu wa Jeshi la Polisi Mstaafu, IGP Said Ally Mwema, Balozi David Kapya, Mwanadiplomasia na Balozi Mstaafu, pamoja na Dk. Stergomena Lawrence Tax, Katibu Mtendaji Mstaafu wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC).




