Na NASRA KITANA
BAADA ya kupoteza bao 1-0 dhidi ya Liechtenstein, Kocha wa Taifa Stars, Miguel Gamondi, ameomba radhi kwa mashabiki kufuatia wachezaji wake kushindwa kutumia vyema nafasi walizozipata.
Pia, ameahidi kwenda kufanyia kazi upungufu uliojitokeza katika mchezo huo.
Taifa Stars ilikubali kichapo cha 1-0 mbele ya Liechtenstein katika mchezo wake wa michuano ya FIFA Series 2026 uliochezwa Uwanja wa Pele, Kigali nchini Rwanda.
Akizungumza baada ya mchezo huo, Gamondi alisema kuwa bado timu yake ina tatizo la umaliziaji jambo ambalo linampa shida, hivyo anahitaji kupambana zaidi ili timu iweze kufanya vizuri na kufunga mabao mengi.
Alisema kuwa anajiskia maumivu kwa ajili ya Watanzania kwani aliwapa matumaini makubwa lakini hawakuweza kutimiza malengo, anaahidi kurekebisha mapungufu na kuwapa furaha mashabiki wa Stars.
“Kwanza niombe radhi kwa mashabiki wetu kwani wachezaji wangu walishindwa kufanya vizuri, tuna tatizo katika nafasi ya ushambuliaji kwani tunashindwa kutumia nafasi ambazo tunazitengeneza, najiskia vibaya lakini tutakwenda kufanyia kazi mapungufu yote yaliojitokeza,” alisema Gamondi.
Gamondi alisema kuwa timu imecheza vizuri lakini haikufikia malengo waliyojiwekea, wanajipanga upya kwa ajili ya mchezo utakaofuata dhidi ya Macau.
Naye kiungo wa Taifa Stars, Novatus Dismas aliomba radhi kwa matokeo ya hayo na kusisitiza, kupoteza kwa mchezo huo ni aibu kwao.
Alisema kuwa pamoja na kucheza vizuri lakini makosa yao ndiyo yaliwagarimu na kushindwa kufanya vizuri sababu walijua mpinzani ni mwepesi.
“Tulicheza taratibu sana mwanzoni mwa mchezo na tumekuja kushtuka baada ya kufungwa bao, tulihisi ni mpinzani ambaye tunaweza kucheza naye na kumfunga tunavyoweza, hii ni aibu kwetu lakini tutaenda kufanya marekebisho ili kuweza kufanya vizuri mchezo ujao,” alisema Novatus.
Nyota huyo alisema kuwa wanakwenda katika mchezo mwingine wakiwa na matumaini ya kupata ushindi.
Hii ni mara ya pili Stars inashiriki michuano hiyo ambayo imekuwa ikisimamiwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), mara ya kwanza timu hiyo ilipoteza dhidi ya Bulgaria kwa bao 1-0 na kushinda dhidi ya Mongolia kwa mabao 3-0.
Sasa hivi Stars ambayo inashika nafasi ya 110 katika viwango vya FIFA itacheza mchezo dhidi ya Macau ambayo katika mchezo wake dhidi ya Aruba ilipoteza mabao mabao 4-1, wakati Liechtenstein ikivaana na Aruba mechiu zote zitachezwa kesho.




