Na NASRA KITANA
BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imemshushia ‘rungu’ kipa wa Yanga, Djigui Diarra, kufuatia matukio ya utovu wa nidhamu aliyoyaonesha katika mechi dhidi ya Mtibwa Sugar iliyofanyikia Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisa Hbari wa TPLB, Karim Boimanda, Diarra amefungiwa michezo mitatu na kutozwa faini ya sh. milioni mbili kwa kosa la kumshambulia mwamuzi wa kati wa mchezo huo, Gilbert Mrina mara baada ya kumalizika.
“Adhabu hiyo ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41:5(5.3) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji.
“Lakini pia Diarra ametozwa faini ya sh. milioni mbili kwa kosa la kuonesha kidole cha kati wakati akitoka uwanjani baada ya kumalizika kwa mchezo huo.
“Diarra ametenda kosa kwa mujibu wa Kanuni ya 41:5(5.4) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji, kwa sababu kitendo hicho kinaashiria matusi na dharau,” alisema Boimanda.
Hata hivyo, taarifa hiyo ilisema mwamuzi wa kati wa mchezo huo Mrina kutoka Kilimanjaro, ameshushwa daraja la uamuzi kwa kosa la kushindwa kuchukua hatua stahili kwa mchezaji Diarra kwa kitendo chake cha utovu wa nidhamu (kumshambulia mwamuzi) kama ilivyoainishwa katika Kanuni ya 42:1(1.6) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Waamuzi.
Taarifa hiyo ilieleza adhabu hiyo imetolewa kwa kuzingatia kuwa ni kosa la kujirudia ambapo mwamuzi Mrina alitenda kosa la aina hiyo katika mchezo namba 65 wa Ligi Kuu kati ya Mbeya City vs Namungo na akaadhibiwa kwa kufungiwa mizunguko mitatu.
Wakati huo huo, TPLB imetoa adhabu kwa klabu ya Simba kwa kuitoza faini ya sh. milioni 10 kufuatia utovu wa nidhamu wa mashabiki wake.
Adhabu hiyo imetokana na tukio la mashabiki wa Simba kuwarushia chupa za maji waamuzi wa mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Pamba Jiji, uliomalizika kwa sare ya 1-1.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa kosa hilo la pili kwa Simba ndani ya miezi miwili kwa mashabiki wake kufanya hivyo, baada ya tukio kama hilo kutokea Februari 25 dhidi ya Dodoma Jiji na adhabu hiyo imetolewa chini ya Kanuni ya 47:1 kuhusu Udhibiti kwa Klabu.




