Na Saray Shabaly
SERIKALI imetangaza watoto wenye miaka sifuri hadi 10 wanatapatiwa chanjo ya polio. Tayari utolewaji wa chanjo hiyo unaendelea katika mikoa mbalimbali nchini, lengo likiwa ni kuutokomeza ugonjwa huo nchini.
Mikoa saba ya Mara, Mwanza, Shinyanga, Kagera, Simiyu na Geita ndiyo inahusika zaidi baada ya kubainika kwa kirusi cha polio katika sampuli za maji machafu mkoani Mwanza.
Habari njema ni kwamba licha ya kugundulika kwa kirusi hicho, hakuna mtu aliyeripotiwa kuugua polio na mara ya mwisho ugonjwa huo kuripotiwa kuwepo nchini, ilikuwa Julai 1996.
Uchanjaji unaoendelea ni tahadhari ya kuepuka kulipuka na kuenea maradhi hayo hatari.
Ofisa wa Ofisi ya Mpango wa Taifa wa Chanjo, Dk. Tumaini Haonga, amekaririwa na vyombo vya habari akisema kutolewa kwa chanjo hiyo, kunatokana na utafiti uliobaini kuwepo kirusi kinachosababisha ugonjwa huo katika baadhi ya mikoa nchini.
“Kila mtoto atakayepata chanjo atawekewa alama maalumu ili kuepuka kurudiwa. Maandalizi yanaendelea vizuri, tunachohitaji ni ushirikiano wa jamii,” amesema Mratibu wa Huduma za Chanjo Mkoa wa Mara, Flowina Muuzaji.
UFAHAMU UGONJWA WA POLIO
Wataalamu wa afya wanaeleza polio ni tishio kwa maisha ya wanadamu na huenezwa na kirusi kinachojulikana kwa jina la ‘poliovirus’, pia ni maradhi yanayoambukiza.
Watu walio katika hatari kubwa ya kuupata ni watoto walio na umri chini ya miaka mitano.
Polio husababisha ulemavu kwa sababu unashambulia mfumo wa neva wa mwanadamu.
Virusi vya polio hushambulia uti wa mgongo na ubongo wa mtu aliyeambukizwa na kumsababishia mwili kupooa. Katika baadhi ya wagonjwa, polio inaweza kusababisha ulemavu wa kudumu.
Tangu kugundulika na kuanza kutumika kwa chanjo ya polio mwaka 1953, matukio ya watu kuugua maradhi hayo duniani yamepungua kwa kiasi cha kutia moyo, ndiyo maana serikali inasisitiza watoto kuchanjwa.
KUMJUA MTU MWENYE POLIO
Mtu anaweza kuzigawa dalili za polio katika aina mbili; ya kupooza na isiyo ya kupooza, kwani baadhi ya wanaoambukizwa virusi vya polio hupata polio ambayo haisababishi kupooza. Hawa huona dalili zisizo kali, ambazo huweza kufanana na zile za mafua na dalili za magonjwa mengine ya virusi.
Hata hivyo, dalili za polio ambazo zinaweza kudumu kwa zaidi ya hata siku 10 ni uchovu, homa, maumivu ya kichwa, koo, kutapika, maumivu ya shingo na kukakamaa, maumivu ya mgongo na kukakamaa, kupungua uzito, maumivu katika mikono au miguu.
Dalili za polio ya kupooza ni zaidi ya hizo kwani mgonjwa hupoteza mjongeo wa viungo vya mwili, maumivu makali ya misuli au kudhoofika, miguu kulegea na kukosa hisia; ambapo ndiyo kupooza kwenyewe.
Dalili zingine ni misuli kupoteza uthabiti kwa kuwa midhaifu, matatizo ya kupumua au kumeza, matatizo ya kupumua mtu awapo usingizini, mwili kushikwa na baridi.
Mtu aweza kuambukizwa polio kupitia njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na kwenda kwenye eneo lenye mlipuko wa maradhi hayo, kugusana na kinyesi cha mgonjwa wa polio, chafya na matone ya kikohozi.
Polio inaweza kuzuilika kwa kuepuka njia zinazosababisha mtu kupata polio. Hata hivyo, njia bora ya kuzuia ni chanjo ya polio. Chanjo hiyo inaweza kuwalinda watoto kwa kuifanya miili yao kuwa na uwezo wa kupambana na virusi vya polio.
Watoto wanapaswa kupatiwa kipimo cha chanjo ya polio kutoka miezi miwili hadi miaka sita. Kawaida chanjo ya polio ya matone mdomoni mara mtoto azaliwapo.
Polio ni ugonjwa hatari ambao unaweza kuharibu maisha, matarajio, na matumaini ya watoto. Chanjo ya polio inaweza kuzuia ugonjwa huo kwa ufanisi. Kwa bahati mbaya, mgonjwa wa polio hawezi kuponywa ulemavu.
IMANI ZA KISHIRIKINA
Katika jamii nyingine, baadhi ya watu huamini uchawi na ushirikina, matokeo yake ni wagonjwa wa polio kuzungushwa kwa waganga wa kienyeji badala ya kupelekwa katika vituo vya afya.
Kwamba, mtu akiugua amelogwa! Badala ya kupelekwa kwa daktari haraka, atazungushwa kwa kina ‘sangoma’ akipigiwa ramli za kutafuta mchawi nani, huku akiendelea kudhoofika.
Katika kutangatanga huko, hali ya mgonjwa huendelea kuwa mbaya na kwa kuwa maradhi hayo huambukiza, watu wengine nao huwa katika hatari ya kuugua na matokeo yake kuwa na watu wenye ulemavu wengi na mbaya zaidi vifo.
Hivyo basi, ni muhimu watu wakaachana na imani za kulogwa katika zama hizi za maendeleo ya sayansi na tekinolojia. Polio ni maradhi yanayoshughulikiwa kisayansi na madaktari katika zahanati, vituo vya afya na hospitali.
Ni vyema mgonjwa akaonwa na madaktari na siyo kupoteza rasilimali za familia kwa waganga na ‘kukamatana uchawi’ katika masuala na matattizo yanayohitaji ufumbuzi wa kisayansi.
Takwimu za Shirika la Afya Duniani zinaeleza zaidi ya asilimia 95 ya watu barani Afrika wamepatiwa kinga ya ugonjwa huo. Hilo lilikuwa moja ya masharti kabla ya kulitangaza bara hilo kufaulu kudhibiti polio.
Chanjo ya polio muhimu kunusuru watoto kupooza




