Na MWANDISHI MAALUMU,
Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji kuvutia wawekezaji wengi wenye mitaji mikubwa kuja kuwekeza nchini.
Alisema hayo, alipoifungua rasmi Hoteli ya Tembo Kiwengwa Resort, iliyopo Kiwengwa, Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Dk. Mwinyi alisema sekta ya utalii, inaendelea kukua kwa kasi kubwa, tayari Zanzibar imevuka rekodi ya wageni wanaoingia nchini, hadi kufikia Oktoba, mwaka huu, takriban 743,000 waliwasili nchini.
Kwa mujibu wa Dk. Mwinyi, hali ya utulivu na amani iliyopo kabla na baada ya uchaguzi mkuu, ni kichocheo kikubwa kinachowavutia wageni kuitembelea Zanzibar.
Rais Mwinyi alisisitiza azma ya serikali ya kufikia wageni milioni moja kwa mwaka.
Akizuingumzia hoteli hiyo, Dk.Mwinyi alielezea kufurahishwa kuona wawekezaji wazawa wanawekeza miradi mikubwa yenye tija na kuwataka wawekezaji wengine kuwekeza zaidi.
Dk. Mwinyi alisema wawekezaji wa aina hiyo, wanachangia dhamira ya serikali ya kufikia lengo la kuzalisha ajira 350 kwa vijana kama ilivyoainishwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kasi ya uwekezaji ni kubwa hivi sasa.
Aliipongeza menejimenti ya hoteli hiyo kwa kuwaunga wajasiriamali wa eneo la Kiwengwa kwa kuwapa soko la uhakika la kuuza bidhaa zao katika hoteli hiyo.




