Na VICTOR MKUMBO
MWENYEKITI wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Crescentius Magori amefunguka kwamba wanachama wa klabu hiyo wamekubaliana na mapendekezo ya kubadilisha katiba.
Mwishoni mwa wiki ulifanyika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Simba, katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na mamia ya wanachama kutoka maeneo mbalimbali.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Magori alisema wanachama wamekubaliana mapendekezo ya kubadilisha kunakuwa na mabadiliko yakiwemo ya mfumo wa uendeshaji.
Alisema alifuatilia vyema mkutano huo na anaamini watafikia malengo waliyojiwekea ikiwemo mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji na baada ya mabadiliko ya katiba kukamilika, wanachama wataanza kuona matunda ya wawekezaji ikiwemo usajili wa aina yake.
“Hivi sasa tutaendelea kuingiza wanachama wapya na usajili utakamilika na wanachama wataanza kuona mambo makubwa ikiwemo uwekezaji,katika mkutano wa mwaka, baadhi ya wanachama hawakuelewa utaratibu kwani waliulizwa kama kuna maswali wakaanza kupiga makofi kitu kilichotafsiriwa na Mwenyekiti wa Klabu Murtaza Mangungu kuwa kila mmoja ameridhika.
“Wanachama wa Simba wamekubali mapendekezo ya bodi ya kufanya marekebisho ya katiba, tutaendelea kusajili wanachama wapya na mwekezaji ataanza kufanya mambo makubwa zaidi,”alisema.
Kiongozi huyo alifafanua kuwa wanachama wanatakiwa kuwa watulivu kuhakikisha Simba inafikia malengo waliyojiwekea.
“Pale kama kuna mtu ambaye alikuwa na swali angenyoosha mkono ndiyo utaratibu,” alisema.
Kuhusu timu kupoteza mechi mbili mfululizo za michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL), Magori alisema wanachama hawatakiwi kukata tamaa kwani uongozi utaendelea kutekeleza yale yote wanayohitaji.
Pia, alisema wachezaji na benchi la ufundi, wameona dosari katika mechi mbili za kimataifa walizopoteza hivyo watafanya kazi ya kuondoa kasoro zilizojitokeza kuhakikisha timu inashinda michezo yote iliyobaki.
Alisisitiza kwamba timu ilipoteza mechi mbili kutokana na wachezaji kushindwa kutumia nafasi walizozipata, lakini ni sehemu ya mpira.
“Tumepoteza mechi mbili hatukuwa na siku nzuri kwa Dar es Salaam na baadaye Bamako, hivyo wachezaji walishindwa kutengeneza nafasi walizotengeneza, hivyo tunaamini yatafanyika maboresho kuhakikisha timu inafanya vyema katika mechi nne zilizobaki,” alisema.
Simba ilipoteza mechi mbili za CAFCL msimu huu kufuatia kufungwa bao 1-0 dhidi ya Petro Atletico ya Angola katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, kabla ya mwishoni mwa wiki kufungwa 2-1 mbele ya Stade Malien, Uwanja wa 26 du Mars, Bamako nchini Mali.
Katika msimamo wa kundi D, Simba inaburuza mkia bila alama yoyote, likiongozwa Petro Atletico kwa pointi nne sawa na Stade Malien zikitofautiana mabao ya kufunga na kufungwa huku Esparance ikishika nafasi ya tatu kwa pointi zake mbili.




