Na AMINA KASHEBA
TIMU ya soka ya TRA United chini ya Kocha Etiene Ndayiragije kesho itaanza mazoezi ya kujiandaa kwa mechi mbalimbali ikiwemo Ligi Kuu Tanzania Bara.
Akizungumza na UHURU, Ofisa Habari wa klabu hiyo, Christina Mwagala, amesema baada Ligi Kuu Tanzania Bara kusimama kupisha michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON), kikosi chao kitatumia muda huo kujiandaa vyema.
Amesema wachezaji walipewa mapumziko ya siku 10 na sasa wanarejea mazoezi kujiandaa vizuri kwa Ligi Kuu pamoja na Kombe la Shirikisho.
“Baada ya mapumziko ya siku 10 wachezaji wanaingia kambini Jumatano (kesho), ambapo mazoezi rasmi yamepangwa kuanza keshokutwa mkoani Tabora, kuhusu tetesi juu ya kusaka saini ya mchezaji wa Yanga, Denis Nkane na kuachana na Emmanuel Mwanengo, hivi sasa siwezi kuongea maana hizo ni tetesi.
“Uongozi utasema kila kitu ni wachezaji gani tumesajili na wangapi tumeachana nao, lakini siyo hivi sasa maana katika usajili kila kitu kinaongelewa sio hapa nchini hadi nje ya nchi sio jambo la ajabu,” amesema.
Msemaji huyo amesema hivi sasa kikosi chao kimeimarishwa zaidi baada ya uwepo wa kocha, Ndayiragije katika kikosi hicho.
“Hivi sasa timu yetu imeimarika kwa kiwango kikubwa tuna imani wachezaji watakuwa bora zaidi, mashabiki wategemee mambo mazuri kwani tunakuja kufanya vitu vikubwa zaidi,” amesema.
Katika Ligi Kuu Bara, TRA United ipo nafasi ya 10 ikiwa na alama tisa katika mechi saba.




