Na ELIZABETH JOHN
LISHE bora ni suala muhimu katika maisha ya kila siku ya binadamu kwa kuwa, husaidia kujiepusha na magonjwa hatari yasiyoambukiza kama moyo, kisukari, figo, presha na kansa.
Pia, wataalamu wanashauri mtu akimaliza kula usiku, angalau asubiri saa moja (Dakika 60) au saa mbili (Dakika 120), kabla ya kulala.
Wanaeleza kuwa, ulaji wa mlo kamili kila siku, ndiyo msingi mzuri wa afya bora kwa kila binadamu.
Lishe ni matokeo ya hatua mbalimbali kuanzia chakula kinapoliwa, kinaposagwa, kumeng’enywa na kufyonzwa mwilini kujenga afya bora.
Lishe bora inahusisha kula mlo kamili, lakini imekua tofauti kwa baadhi ya familia nyingi za kitanzania, ambapo idadi kubwa hawapati chakula bora chenye kutosheleza.
Makundi ya chakula ni nafaka, mizizi na ndizi mbichi, vyakula asili ya nyama na jamii ya mikunde, mbogamboga, matunda na kundi la mwisho ni mafuta, sukari na asali.
Hata hivyo, imejengeka tabia baadhi ya watu kutokula kwa muda sahihi, hatua ambayo husababisha ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza.
Inaelezwa mfumo wa maisha, umechangia kwa kiasi kikubwa jamii kutofuata mtitiriko mzuri wa ulaji hususan watu wanaoishi mijini ambao idadi kubwa ni wafanyakazi na wafanyabiashara.
Idadi kubwa ya jamii inayoshi mijini, haina ratiba kamili ya ulaji chakula, kitendo kinachosababisha ongezeko la magonjwa yasiyo ya kuambukiza kama alivyoeleza Ofisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Husna Faraji.
Utaratibu wa kulala muda mfupi baada ya kula chakula cha usiku, umeelezwa una madhara makubwa kwa afya ya binadamu na anashauri baada ya kula, mtu angalau asubiri kwa saa moja (Dakika 60) au mbili (Dakika 120), kabla ya kulala kuepukamagonjwa hatarishi kama moyo, kisukari na kuvuruga mfumo wa mmeng’enyo wa chakula.
Madhara mengine ni gesi kujaa tumboni, uzito mkubwa, shinikizo la juu la damu, chembe ya moyo na chakula kushindwa kusagika vizuri tumboni.
Akizungumza na UHURU, Ofisa Lishe, Husna alisema tafiti zinaonesha kulala muda mfupi, baada ya kula, husababisha chakula kushindwa kuyeyushwa kwa ufanisi unaotakiwa mwilini.
Alisema kuwa, ingawa mtu hawezi kuona madhara ya haraka, tabia hiyo, hujenga mazingira ya mwili kupata magonjwa yasiyoambukizwa muda mrefu.
“Hakuna madhara makubwa kwa wakati huo, lakini baadaye, anaweza akapata magonjwa ya kisukari na moyo, kutokana na chakula kutokuwa katika mfumo mzuri wa kusagika hivyo kubaki tumboni,” alisema Husna.
Alisema anayelala mara baada ya kula, huanza kuonesha dalili za kutokuwa na afya bora, ikiwemo kupata chembe ya moyo mara kwa mara, hatua inayomfanya ashindwe kufanya shughuli zake kwa ufanisi.
“Unapokuwa na uzito mkubwa na kukaa bila kuushughulisha mwili, huo ni mwanzo wa kupata magonjwa makubwa yasiyoambukizwa kama shinikizo la damu na matatizo ya moyo,” alisema.
Husna alisema njia bora baada ya kula chakula hasa usiku, anatakiwa kupata muda wa kutosha chakula kisagike vyema tumboni.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Elimu na Mafunzo ya Lishe kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC), Dk. Esther Nkuba, alisema kulala muda mfupi baada ya kula usiku, kuna madhara mengi.
Daktari huyo, alisema ni muhimu kuwa makini unapokula chakula cha usiku, kuepusha madhara baadaye.
Wakati Dk.Nkuba akitoa maelezo hayo, Ofisa Lishe Mwandamizi kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani, Fatma Mwasora, alisema kiwango kingi cha chakula hasa cha jioni(usiku), huhifadhiwa kama mafuta kwa sababu wakati wa kulala mchakato wa chakula mwilini hufanyika taratibu, hivyo ni muhimu kula kidogo.
“Chakula cha jioni ni vizuri kiliwe kabla ya saa moja jioni, mlo uwe mwepesi, usiwe na virutubishi vya aina ya nishati lishe au wanga kwa wingi, kwasababu umeng’enywaji wake hufanyika taratibu sana. Pia, mlo uwewa mchanganyiko wa makundi yote na uwe na mboga nyingi zaidi ikiwa ni pamoja na matunda.
Inashauriwa baada ya mlo wa jioni kusubiri angalau kwa saa mbili au tatu kabla ya kulala na muda huo,unaweza kutumia kufanya mazoezi ya kushughulisha mwili kamakutembea, kudeki, kuosha vyombo au kufagia,” alisema.
Alisema mara nyingi mtu anapolala muda mfupi baada ya kula, mfumowa usagaji chakula hufanya kazi taratibu na wakati huo mwili huchochewa kumwaga asidi tumboni.
Fatma, alisema hatua hiyo, husababisha chakula kubaki tumboni muda mrefu na kusababisha kuwepo asidi katika utumbo na hata kuingia kwenye mfumo wa chakula hasa sehemu za koo.
“Tafiti kadhaa zinaonesha kuna ongezeko la utolewaji asidi ya tumbo baada ya kulala na hivyo, kusababisha hali ya koo kukereketa na hata kusababisha kiungulia na madhara mengine,” alisema.
NINI CHA KUFANYA
Fatma, alisema ili kuepuka matokeo mabaya, inashauriwa kusubiri angalau saa mbili hadi tatu (Dakika 90), baada ya kula kabla ya kwenda kulala, kuupa mwili muda wa kutosha kusaga chakula.
“Tunashauriwa kula mapema kupunguza ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza kamauzito mkubwa au kiribatumbo, kisukari na kusababisha ongezeko la vifo ambavyo vinaweza kuzuilika,” alisema.
Alishauri kufanya mazoezi ya kushughulisha mwili kama kuendesha baiskeli, kudeki, kuosha vyombo, kutembea, kucheza muziki na mazoezi mengine mepesi ya mwili yakulinda afya.
“Kama utachelewa kula chakula cha jioni, ni vyema mlo wako, uwe mwepesi kama vile mboga kwa wingi, vyakula vya aina ya protini au matunda na si zaidi ya aina mbili
“Kuzingatia ulaji unaofaa, kunaweza kusaidia kuwa na uzito sahihi wa mwili na kutuepusha na magonjwa yasiyoambukiza,” alisema mtaalamu huyo.
WANASAIKOLOJIA
Katibu Mkuu wa Chama cha Wanasaikolojia Tanzania (TAPA), Albano Michael, alisema ulaji huo, pia huathiri afya ya akili na tabia za binadamu hasa pale inapofanywa kwa muda mrefu na kuwa mazoea katika maisha.
Kwa mujibu wa taaluma ya saikolojia, binadamu huongozwa na tabia alizojijengea na mifumo ya akili iliyojengeka muda mrefu, hali inayofanya ratiba ya kula na kulala kuwa sehemu ya mfumo wa maisha ya mtu.
Alieleza mtu anayezoea kula muda fulani kila siku, ubongo wake hujijengea mpangilio maalumu unaoashiria kuwa huo ndiyo muda sahihi wa kula, hatua inayosababisha ubongo kutoa taarifa za njaa hata kama mazingira hayaruhusu.
“Mfumo wa akili una mizunguko ya umeme na kemikali ambazo hujitokeza moja kwa moja.
“Mtu akizoea kula kisha kulala mara moja, ubongo huanza kuutambua huo kama mfumo wa kawaida wa maisha,” alisema.
Alisema tabia hiyo inapobadilishwa ghafla, mwili hulazimika kutumia nguvu nyingi kujaribu kurekebisha mfumo wake wa ndani, hali inayoweza kuathiri mmeng’enyo wa chakula, usingizi na ustawi wa kisaikolojia.
Mwanasaikolojia, Magdalena Ngenzi, alisema ulaji huo husababisha ubongo na mwili kufanya kazi kwa mkanganyiko, jambo linaloweza kuleta mabadiliko ya kibailojia na kimwili yasiyokuwa ya kawaida.
“Unapotoka nje ya ratiba na kubadilisha ratiba, utalazimisha mwili kufanya kazi kinyume na ulivyozoea, kuna mabadiliko yanatokea, siyo tu mwilini, katika akili, kwa sababu utendaji wa akili unategemea sana mpangilio wa kawaida wa mwili,” alisema.
Mwanasaikolojia huyo, alisisitiza wananchi wanapaswa kuzingatia ratiba sahihi ya kula na kulala kwa muda sahihi kwa kuwa, kuishi bila mpangilio,huathiri afya ya akili, tabia, mwili na kusababisha matatizo makubwa ya kiafya na kisaikolojia.




