Na MWANDISHI WETU
RAIS wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), Gianni Infantino, amesema shirikisho hilo lipo tayari kushirikiana na Tanzania katika programu zake za maendeleo kusaidia kutengeneza fursa kwa vijana kunufaika na mpira wa miguu.
Pia, Infantino alisema hatua hiyo itasaidia ujenzi wa miundombinu na uendelezaji wa vituo vya ufundi.
Infantino aliyazungumza hayo jijini Rabat, Morocco, alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda na ujumbe wake.
Rais huyo wa FIFA, aliipongeza Tanzania kwa kazi kubwa iliyofanywa na inayoendelea kufanywa na serikali katika ujenzi wa miundombinu ya michezo kuelekea Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027 na shirikisho hilo litaunga mkono jitihada hizo.
Kwa upande wake Waziri Makonda alimshukuru Infantino kwa ushirikiano mkubwa anaoutoa kwa Tanzania katika maendeleo ya mpira wa miguu na amemhakikishia kuwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na serikali anayoiongoza inaunga mkono jitihada hizo na ipo tayari kushirikiana na FIFA.
Aidha, Makonda alimkaribisha Infantino kutembelea Tanzania, huku akisisitiza kuwa Tanzania ipo tayari kuwa mwenyeji wa matukio mbalimbali ya FIFA ikiwemo mashindano mbalimbali, mikutano na ziara za viongozi na wataalamu.




