Na MUSSA YUSUPH, Dodoma
KAMATI ya Kudumu ya Bunge, Viwanda, Biashara, Kilimo na Ufugaji, imeishauri serikali kupitia Wakala wa Vipimo (WMA), kuanza kuhakiki vipimo vinavyotumika katika muda wa maongezi na bando za intaneti.
Pia, imeishauri Wizara ya Viwanda na Biashara na Wizara ya Nishati, kuhakikisha mita zote mpya za umeme zinahakikiwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo kabla ya kusimikwa kwa watumiaji.
Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mariam Ditopile, aliyasema hayo bungeni jijini hapa jana, alipowasilisha taarifa kuhusu utekelezaji majukumu ya Wizara ya Viwanda na Biashara (Fungu 44) kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 na maoni ya kamati kuhusu makadirio ya mapato na matumizi mwaka wa fedha 2026/2027.
Ditopile alisema kumekuwepo na malalamiko ya wananchi, kuhusu thamani halisi za matumizi ya huduma za muda wa maongezi na bando za intaneti.
“Kamati inaishauri wizara kupitia WMA kuanza jukumu la kuhakiki vipimo vinavyotumika kwenye muda wa maongezi na bando za intaneti, ili wananchi waweze kupata thamani halisi ya huduma wanazolipia,” alisema.
AGIZO MITA ZA UMEME
Ditopile ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kondoa Mjini (CCM), alisema kuna mwitikio hafifu kutoka kwa baadhi ya wazabuni wanaouza mita za nishati ya umeme katika kutekeleza takwa la kisheria la kuhakiki mita hizo WMA kabla ya kuwasilishwa katika ununuzi.
Makamu mwenyekiti huyo alisema hali hiyo inaathiri usahihi wa ankara, kuibua malalamiko ya walaji na kudhoofisha uadilifu wa mifumo ya mapato.
“Kamati inaishauri Wizara ya Viwanda na Biashara kushirikiana na Wizara ya Nishati, kuhakikisha mita zote mpya za umeme zinawasilishwa ili kuhakikiwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo kabla ya kusimikwa kwa watumiaji,” alieleza.
CHANGAMOTO YA LUMBESA
Kwa mujibu wa Ditopile, changamoto ya lumbesa haijapata suluhu ya kudumu, jambo linalosababisha baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu kuendelea kutumia mfumo huo kuwanyonya wakulima na kuikosesha serikali mapato.
Alisema kamati inaishauri serikali kushirikisha mamlaka zote zinazohusika na vipimo, ili kupata suluhu ya kudumu kwa kuwa usimamizi wa pamoja utasaidia kubaini chanzo cha tatizo na kuweka mkakati madhubuti ya kulidhibiti.
MAONI YA WABUNGE
Akichangia mjadala, Mbunge wa Gairo (CCM) Ahmed Shabiby, alisema vipo baadhi ya viwanda vya kigeni vinazalisha nondo zenye vipimo ambavyo siyo sahihi.
Alisema badala ya wahusika wenye viwanda kukamatwa, lakini wamiliki wa maduka wamekuwa wakikamatwa na kutozwa faini, hivyo kuwarudisha nyuma wafanyabiashara.
“Tuwaangalie wenye viwanda, siyo mnawapiga faini, vifungwe. Vipo viwanda vinavyozalisha nondo feki. Vipo viwanda vya juisi vinaweka picha ya embe lakini ndani ni kemikali. Mgonjwa anapelekewa juisi ya embe lakini kumbe ni kemikali. Hili tuliangalie,” alisisitiza mbunge huyo.
Mbunge wa Buchosa (CCM) Erick Shigongo, alitilia mkazo suala la uwepo wageni wanaofanya biashara zinazowezwa kufanywa na wazawa.
Alisema wizara ihakikishe wageni hawafanyi biashara ambazo zinazoweza kufanywa na wazawa, kwa kuwa wapo baadhi yao ambao wamekuwa wakiwarudisha nyuma wazawa kwa kuuza bidhaa kwa bei ya chini.
Mbunge kutoka Baraza la Wawakilishi, Simai Mohammed Said, alisema katika mkakati wa kupunguza umaskini Zanzibar imechagua maeneo matatu ambayo ni biashara, huduma na utalii.
Mbunge huyo alisema ni muhimu wizara hiyo ikajikita katika maeneo mengine kama ya kilimo na utalii ili kukuza biashara.




