Na AMINA KASHEBA
KOCHA wa Yanga Princess, Edna Lema amewaomba mashabiki wa timu hiyo kujitokeza kwa wingi katika mchezo wa dabi ya Ligi ya Wanawake Tanzania Bara dhidi ya Simba Queens kwa lengo la kuwapa hamasa wachezaji.
Mchezo huo utafanyika kesho saa 12:00 jioni katika Uwanja wa KMC, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza Dar es Salaam, kocha huyo alisema maandalizi ya mchezo wa dabi yanaendelea vizuri huku wachezaji wake wakitambua umuhimu wa mechi hiyo.
“Waje Jumapili tunatamani kushinda mchezo wetu dhidi ya Simba Queens ni kipimo kizuri kwa sisi kuona ni namna gani tunaenda kujipanga kujiandaa vizuri msimu huu, hivyo ni mechi muhimu kwetu.
“Nawahaidi tunaenda kufanya vizuri katika mchezo huo kwa sababu tunahitaji kupata ushindi ili kuendelea kubaki kileleni kwa sababu sisi ndiyo tunaongoza ligi hivi sasa,” alisema.
Kocha huyo aliongezea kuwa wachezaji wake wako tayari kwa mchezo wa kesho hivyo anawaomba wadau wa soka wajitokeza kwenda kuona burudani kutoka kwao kwani wamejipanga vyema.
“Tunawaomba mashabiki wa Yanga princess kujitokeza kuja kutupa sapoti ili kufanya vizuri katika mchezo wetu, malengo yetu ni kuendelea kuwa kileleni katika msimamo wa ligi, mechi ya leo ndiyo italeta njia nzuri,” alisema.
Katika msimamo wa ligi Yanga Princess ipo kileleni akiwa na pointi 12, wakati Simba Queens yupo nafasi ya pili akiwa na pointi 12 wote wameshuka dimbani mara nne.




