Na AMINA KASHEBA
NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, amewataka wachezaji wa timu ya taifa ‘Taifa Stars’, kutoka tamaa isipokuwa wapambane kupata ushindi katika mechi ijayo.
Taifa Stars itacheza na Tunisia kesho katika mechi ya mwisho ya kundi C ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 itakayopigwa Uwanja wa Prince Moulay Abdellah, Rabat.
Tanzania ilianza michuano hiyo kwa kichapo dhidi ya Nigeria (2-1) na sare ya bao 1-1 ilipocheza na Uganda.
Akizungumza kutoka Morocco juzi, Naibu Waziri huyo alisema Taifa Stars inapaswa kupata ushindi dhidi ya Tunisia, kuhakikisha inatinga hatua ijayo.
“Kila mmoja alitarajia ushindi, tumeona wenzetu wamejipanga, msikubali kukataa tamaa, mechi yetu dhidi ya Tunisia twendeni tukapambane tukapate pointi tatu.
“Twendeni tukawape zawadi Watanzania, zawadi ya mwaka mpya kwa kuwafunga Tunisia, serikali ipo na nyinyi na wananchi wa Tanzania bado wapo na nyinyi, nendeni mkapambane,” alisema.
Mchezaji wa Stars, Simon Msuva ambaye alikuwa mchezaji bora dhidi ya Uganda, alisema bado wana imani watafanya vizuri dhidi ya Tunisia.




