Na MWANDISHI WETU
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, amezindua namba maalumu, itakayotumiwa na wananchi kufuatilia Kitambulisho cha Taifa baada ya kuwasilisha maombi ya kitambulisho.
Hatua hiyo itatoa fursa kwa wananchi kupata na kujua taarifa za maombi ya kitambulisho kwa kutumia namba hiyo maalumu.
Waziri huyo alizindua namba hiyo maalumu Dar es Salaam, ambapo alisema vitambulisho vingi vimezalishwa na tayari vimepelekwa sehemu husika zikiwemo wilayani.
“Hivi leo tunavyozungumza katika wilaya zetu zote nchini, viko vitambulisho vingi sana ambavyo havijachukuliwa na sababu kubwa mwombaji hajui kitambulisho chake kipo katika hatua gani
“Kupitia mfumo huu ambao ninauzindua, utajibiwa na utaambiwa kama namba yako umepata ndani ya siku tano na kama hujapata ndani ya siku tano tangu ulipoomba ukitumia mfumo huu (15274) utajibiwa kwanini hujapata,”alisema Waziri Simbachawene.
Aliongeza pia serikali inafikiria kusitisha matumizi ya namba ya utambulisho (NIN), kwasababu watu wengi wameacha kwenda kuchukua vitambulisho.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), James Kaji, alisema mamlaka imeendelea kushusha vitambulisho hadi ngazi ya kata, lakini bado wananchi hawajavifuata kabla ya kuvipeleka wilayani.
Alisema baada ya kuvipeleka wilayani, anaamini kupitia mfumo huo mpya wa namba 15274, vitambulisho vitaendelea kufuatwa kwa kuwa umerahisisha zaidi taarifa za mwombaji kupitia simu ya mkononi.




