Na MWANDISHI WETU
SOKA la Tanzania limezidi kupiga hatua siku hadi siku kuanzia ngazi za klabu ya timu ya taifa.
Hilo limethibitishwa wiki iliyopita baada ya Taifa Stars kuandika historia ya kutinga kwa mara ya kwanza hatua ya mtoano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025.
Taifa Stars iliweka historia hiyo kwa kanuni ya ‘best looser’ baada ya kumaliza nafasi ya tatu katika kundi C la AFCON 2025 ikiwa na alama mbili kufuatia kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Tunisia katika mtanange wa mwisho wa makundi uliopigwa Uwanja wa Prince Moulay Abdellah jijini Rabat, Morocco.
Timu hiyo jana ilishuka dimbani kuvaana na Morocco katika hatua ya 16 bora iliyopangwa kupigwa Uwanja wa Prince Moulay Abdellah.
Ikiwa moja kati ya miamba 16 iliyotinga mtoano, mafanikio hayo yameifanya Stars kuweka rekodi hiyo kwa mara kwanza huku Kocha Muargentina Miguel Gamondi akivunja mwiko wa miaka 45, uliowashinda makocha watano tofauti waliowahi kuinoa timu hiyo.
Makocha hao ni Mpoland Slawomir Wolk aliyeinoa Stars katika fainali za mwaka 1980, Emmanuel Amunike raia wa Nigeria (2019), Adel Amrouche kutoka Algeria na Mtanzania Hemed Morocco katika fainali za mwaka 2023, ambao wote vikosi vyao viliishia makundi.
Mwaka 1980, Wolk aliiongoza Taifa Stars katika mechi tatu ikifungwa mbili na kutoka sare moja wakati mwaka 2019 Mnigeria Amunike aliiongoza Stars kufungwa mechi zote tatu na kuburuta mkia.
Katika fainali za mwaka 2023, Taifa Stars chini ya Amrouche na baadaye Morocco, ilimaliza nafasi ya tatu kwa alama mbili, ikifungwa mechi moja na kutoka sare mbili.
Amrouche aliiongoza Stars katika mechi moja ambayo ilipoteza kabla ya kufungiwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) na nafasi yake kukaimiwa na mzawa Morocco ambaye aliiongoza kupata sare mbili na kurejea nyumbani.
Kwa mujibu wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), michuano ya AFCON inatarajiwa kutumia dau la dola za Marekani milioni 32 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 78.3 za Tanzania kwa ajili ya zawadi pekee.
Katika mchanganuo wa fedha hizo, bingwa wa michuano hiyo anatarajiwa kuvuna dola za Marekani milioni saba ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 17.1.
Timu itakayoshika nafasi ya pili itavuna dola za Marekani milioni nne ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 9.7 za Tanzania.
Timu mbili zitakazoishia hatua ya nusu fainali, kila moja itaondoka na dola za Marekani milioni 2.5 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 6.1 za Tanzania.
Timu nne zitakazoishia hatua ya robo fainali zitavuna dola za Marekani milioni 1.3 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 3.1 za Tanzania.
CAF pia imeeleza kwamba, miamba minane itakayoishia hatua ya 16 bora itavuna dola za Marekani 800,000 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 1.9 za Tanzania.
Timu zitakazoishia nafasi ya tatu katika kundi, kila moja itaondoka na dola za Marekani 700,000 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 1.7 wakati zile zitakazoburuta mkia katika kila kundi zitavuna dola za Marekani 500,000 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 1.2 za Tanzania.
ILIVYOKUWA KUNDI C
Taifa Stars ilipangwa kundi C na timu za Nigeria, Tunisia na Uganda.
Tanzania ilimaliza nafasi ya tatu kwa alama mbili, kinara Nigeria ilikuwa na pointi tisa, Tunisia nafasi ya pili kwa alama nne wakati Uganda ikiburuta mkia kwa pointi moja.
Tanzania ilianza michuano hiyo kwa kichapo cha mabao 2-1 dhidi ya Nigeria kabla ya kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Uganda na 1-1 ilipocheza na Tunisia.
AFCON ZILIZOPITA
Katika fainali zote tatu zilizopita ambazo Stars ilishiriki, timu hiyo haijawahi kutinga hatua ya mtoano hata mara moja.
Katika michuano ya mwaka 1980 iliyofanyika Nigeria, Taifa Stars ilipangwa kundi A na timu za Nigeria, Misri na Ivory Coast.
Taifa Stars iliburuta mkia kwa pointi moja baada ya kutoka sare na Ivory Coast. Awali, ilifungwa mabao 3-1 dhidi ya Nigeria na mabao 2-1 ilipovaana na Misri.
Katika AFCON mwaka 2019 zilizofanyika nchini Misri, Tanzania ilipangwa kundi C na timu za Algeria, Senegal na Kenya.
Taifa Stars ilimaliza katika kundi hilo ikiwa nafasi ya nne baada ya kufungwa mechi zote tatu.
Kikosi hicho kilichokuwa kikinolewa na Amunike, kilianza kwa kichapo cha mabao 2-0 dhidi ya Senegal, kichapo cha mabao 3-2 kutoka kwa Kenya na kichapo cha mabao 3-0 dhidi ya Algeria.
Pia, Taifa Stars iliburuta mkia katika hatua ya makundi ya AFCON mwaka 2023 zilizofanyika nchini Ivory Coast.
Ikiwa imepangwa kundi F, Stars ilivuna pointi mbili (nyingi zaidi ya AFCON ilizoshiriki awali), ikianza kwa kichapo cha mabao 3-0 dhidi ya Morocco, sare ya bao 1-1 kutoka kwa Zambia na suluhu dhidi ya DRC.
TANZANIA ILIVYOFUZU
Taifa Stars ilifuzu fainali hizo baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Guinea katika mchezo wa mwisho wa kundi H, kuwania kufuzu AFCON uliopigwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Bao la mshambuliaji nyota, Simon Msuva katika dakika ya 61, limeipeleka Tanzania katika AFCON baada ya kufikisha pointi 10 na kukwea hadi nafasi ya pili katika kundi hilo.
Msuva aliiandikia Stars bao katika dakika ya 61, akiuweka mpira kimiani kwa kichwa baada ya kuunganisha pasi ya Mudathir Yahya.
Bao hilo liliibua shangwe la aina yake kutoka kwa wachezaji na mashabiki walioujaza uwanja wa Benjamin Mkapa wenye uwezo wa kuingiza watu 60,000.




