Na NASRA KITANA
NYOTA wa muziki wa kizazi kipya, Nasib Abdul ‘Diamond’, ametoa ahadi kwa mashabiki zake kuwa kabla ya mwezi wa mtukufu wa Ramadhani anatarajia kuja kivingine kwa kuachia albamu mpya.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Diamondi alisema kuwa albamu hiyo itakuwa bora na kuwakumbusha mashabiki wake kwanini alipendwa kipindi anaanza muziki.
Alisema kuwa katika albamu hiyo kutakuwa na nyimbo kali tofauti na ‘Zuwena’ na ‘Yatapita’ ambazo tayari zimeshasikilizwa sana na mashabiki wake.
“Natarajia kutoa albamu yangu kabla ya mwezi wa Ramadhani, ninataka niwakumbushe nini kilinifanya niweze kupendwa kipindi naanza muziki na nyimbo zangu kama ‘Kamwambie’ na ‘Mbagala’.
“Albamu itakuwa moto wa kuotea mbali kwani itasheheni nyimbo zenye ubora zaidi tofauti na zilizozoeleka, kila shabiki wangu atasikiliza moja hadi nyingine bila kuchoka,” alisema Diamond.
Msanii huyo alisema anajua nini ambacho mashabiki wake wanakitaka, hivyo atawapatia kabla ya kuanza kwa mfungo wa mwezi wa Ramadhani.
Msanii huyo amewataka mashabiki wake kukaa mkao wa kula kwani albamu hiyo itakata kiu ya burudani waliyoikosa kwa muda mrefu.




