Na NASRA KITANA
WACHEZAJI wa zamani wa Simba, Yanga na Taifa Stars, Abdallah Kibadeni, Sunday Manara na Ally Mayay, wamesema kuwa ni vyema kuitunza amani ya nchi kwani ndiyo msingi wa umoja na mshikamano.
Waliyasema hayo katika hafla ya kuwapongeza wanamichezo waliofanya vizuri katika mashindano mbalimbali ya kimataifa.
Nyota wa zamani wa Simba, Kibadeni, alisema kuwa amani ni jambo la msingi katika nchi, pia linaongeza morari kwa wanamichezo kuweza kufanya kazi zao kwa uhuru na mshikamano.
“Niwaambie tu Watanzania na wanamichezo wote kwa ujumla, amani ni jambo la msingi katika nchi hivyo inapaswa kudumishwa ili kuendeleza mpira wetu wa miguu katika anga za juu zaidi.
Naye nyota wa zamani wa Yanga, Manara alisema kuwa kila Mtanzania anatakiwa kudumisha, kuilinda amani nchini.
Alisema kuwa endapo amani ikikosekana hata mpira hauwezi kuchezekeka ambao ndiyo ajira ya vijana wengi hapa nchini inayowasaidia kuwaingizia kipato.
“Niseme tu kuwa kila mmoja kwa nafasi yake anatakiwa kuilinda na kuithamini amani katika nchi yetu, ikikosekana amani hakuna kitu ambacho kitafanyia ndani ya nchi na hata nchi jirani pia wataogopa kuja kuwekeza na kucheza soka hapa kwetu,” alisema Manara.
Kwa upande wake nyota wa zamani wa Yanga, Mayay alisema kuwa kila mmoja anajua umuhimu wa amani nchini, hivyo Watanzania wanapaswa kuilinda kwa hali na mali.
Alisema kuwa ili wachezaji waweze kuwa huru na kwenda kucheza katika mataifa mbalimbali lazima nchi wanayotoka iwe na amani ili waweze kupata kibali cha kwenda nchi nyingine.
“Tumekuwa tukiheshimika na kuthaminiwa kutokana na Tanzania kujulikana na nchi yenye amani na utulivu, hivyo ni jukumu letu kuilinda kwa hali na mali ili kusitokee na machafuko ambayo yataiharibia sifa nchi yetu,” alisema Mayay.




