Na AMINA KASHEBA
TIMU za Yanga na Azam FC kutoka Tanzania Bara, leo zitashuka katika fainali ya Kombe la Mapinduzi 2026, inayotarajiwa kuwa na ushindani wa hali ya juu.
Miamba hiyo itavaana saa 10:30 jioni katika Uwanja wa Gombani Complex, Pemba.
Yanga imetinga fainali baada ya kuitoa TRA United kwa ushindi wa bao 1-0 wakati Azam FC ikiiondosha Simba kwa ushindi wa bao 1-0, wiki iliyopita.
Akizungumza maandalizi ya mchezo huo, Kocha wa Azam FC, Florent Ibenge, alisema kikosi chake kipo tayari kwa fainali na wamejiandaa kuwa bora uwanjani kuliko wapinzani wao.
Alisema haitakuwa rahisi kwani timu zote zina ubora mkubwa, lakini lengo lao ni kupata ushindi katika mtanange huo.
“Tunajua Yanga ndiyo timu bora zaidi Tanzania hivi sasa, lakini sisi tutakuwa bora zaidi yao kwa sababu tumejipanga kuhakikisha tunafanya vizuri na kutimiza yale malengo yetu ambayo tumejiwekea.
“Wachezaji wote wako tayari kwa mechi, pia ninawaamini watafanya vizuri,” alisema Ibenge.
Nyota wa timu hiyo, Nassor Saadun alisema kila mchezaji amejiandaa vizuri kukabiliana na Yanga katika mchezo huo, watafuata maelekezo ya walimu wao kuhakikisha wanatimiza malengo yao ya kutwaa kombe.
“Malengo yetu ni kuchukua ubingwa wa Mapinduzi tutahakikisha tunacheza vizuri na kuzingatia yale tuliyofundisha katika viwanja vya mazoezi, tunatambua mchezo utakuwa mgumu lakini sisi tutapambana kupata ushindi,” alisema.
Kocha wa Yanga, Pedro Goncalves, alisema maandalizi yako vizuri kuelekea katika fainali hiyo, pia wamejipanga kuchukua ubingwa huo ingawa mchezo utakuwa na ushindani mkubwa.
“Tunatambua fainali itakuwa na ugumu lakini tumejipanga kufanya vizuri na wachezaji wamefanya mazoezi ya kutosha kuhakikisha wanacheza katika kiwango kizuri ambacho kitatupa ushindi,” alisema.
Kocha huyo alisema haijalishi mechi itakuwa na ugumu kiasi gani, lakini watapambana kuhakikisha wanachukua ubingwa huo.




