Na ZIANA BAKARI
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimeridhishwa na mwanzo mzuri wa utekelezaji wa Ilani yake, uliofanyika katika siku 100 za Rais Samia Suluhu Hassan, huku kikiwataka Watanzania, kuaminiana na kuzungumza kwa pamoja kwa kuwa jamii inahitaji maridhiano, siyo fujo.
Hayo yalibainishwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Stephen Wasira, alipofanya mahojiano kupitia kipindi cha mizani cha TBC kilichoangazia siku 100 za Rais Dk. Samia, tangu aingie madarakani baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025.
Alisema utekelezaji wa ahadi hizo, utaendelea kwa kasi, uwazi na uwajibikaji kupitia Rais Samia.
“Rais Dk. Samia, ameonesha dhamira ya dhati katika kusimamia miradi ya maendeleo na kuboresha ustawi wa wananchi, CCM imejijengea heshima kwa kutimiza yale inayoyaahidi na kasi ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo inayoakisi Dira ya Chama katika kujenga uchumi imara na jamii yenye matumaini.
“Agosti 28, mwaka jana, tulizindua kampeni yetu ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2025, tulipokuwa Kawe jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wetu ambaye ndiye Rais wetu, alitoa ahadi alisema wananchi wakimchagua katika muda wa siku 100 kuna mambo atafanya,”
Alisema Rais Samia, aliahidi kuzindua Bima ya Afya kwa Wote, ambapo matarajio ya awali yakitarajiwa kuanza kwa makundi maalumu yakiwemo ya wazee, watoto, wenye ulemavu na wajawazito ambao wataingizwa katika mfumo huo kuhakikisha wanapata huduma za afya kwa uhakika na kwa wakati.
Aidha, alieleza kuwa, serikali itachunguza na kutathimini uwezekano wa kugharimia kwa asilimia 100 matibabu na vipimo vya kibingwa, hususan kwa magonjwa makubwa yasiyoambukiza yakiwemo, figo, saratani, moyo na kisukari.
Alifafanua kuwa, tayari jumla ya sh. bilioni 6.8 zimetolewa katika awamu ya kwanza kwa kuanza kuwahudumia wagonjwa wanaohitaji matibabu ya magonjwa hayo, hatua inayolenga kupunguza mzigo wa gharama kwa wananchi na kuboresha upatikanaji wa huduma bora za afya nchini.
Pia, alisema serikali tayari imeajiri wahudumu wa afya 5,000 wakiwemo wauguzi na wakunga, pia imeendelea kutekeleza agizo la kutozuia maiti katika hospitali mbalimbali nchini.
“Serikali itaandaa mkakati madhubuti wa kisayansi kuhakikisha kila mtoto wa darasa tatu anaweza Kusoma Kuandika na Kuhesabbu ‘KKK’ ambao hivi karibuni Rais Samia alishazindua.
Aidha, alisema sh. bilioni 200 tayari zimetolewa kwa mitaji ya vijana na wanawake, jambo hilo ni muhimu kwa sababu, vijana wanaweza kufungua mitaji na kuanzisha kampuni zao wajiajiri.
Alisisitiza kuwa, serikali itaendeleza jitihada za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia itumike badala ya kuni na mkaa na uhifadhi wa mazingira kama inavyoelekeza Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
“Rais Dk. Samia alisema ataanda mfumo rafiki wa uwajibikiaji ambao mawaziri, wakuu wa mikoa na watendaji wengine watatoa taarifa za kujibu maswali kutoka kwa wananchi kwa njia ya kijijitali au ujumbe mfupi ambao ni kipimo, jambo hilo tayari limeanza.
“Siku 100 Rais Dk. Samia aliahidii kuanzisha mfumo utakaoleta maridhiano, lakini zilipotokea vurugu aliunda tume kujua chanzo na hadi sasa inafanya kazi na ikimaliza itasema. Tunawasihi Watanzania kuaminiana, kuongea kwa pamoja kwa kuwa jamii inahitaji maridhiano na siyo fujo, haki na amani ni kama kuku na yai huwezi kuvitenga hata siku moja,” alisema.




