NA EMMANUEL MOHAMED
SHIRIKA la Masoko la Kariakoo, limesema tayari limetekeleza asilimia 95 ya maagizo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, aliyoyatoa wakati akilifungua soko hilo la kimataifa.
Februari 8, mwaka huu, Rais Samia alitoa maagizo kwa uongozi wa soko ya kujenga jengo la kunyonyeshea watoto na kuhakikisha kunakuwa na usalama wa bidhaa za wafanyabiashara.
Akizungumza na gazeti hili jana, Meneja Mkuu wa Shirika hilo, CPA Ashiraf Abdulkarim, alisema tayari wamewasilisha ombi la bajeti ya kujenga jengo la kunyonyeshea watoto Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).
Abdulkarim alisema baada ya kuwasilisha bajeti hiyo, tayari wataalamu kutoka ofisi hiyo, wakiwemo wahandisi wa majengo na afya, walifika sokoni hapo kutekeleza agizo hilo la Rais Samia.
“Wiki iliyopita, watalaamu hao, walikuja na tukawaonyesha eneo ambalo tumelitenga kujenga jengo hilo na zuri, wamekuja na watu wa afya ambao wao wataona vitu gani vinafaa kuwekwa, huduma za kuonyeshea watoto zitolewe ipasavyo,”alisema
Alisema baada ya hatua hiyo, kinachosubiriwa ni kukabidhiwa mchoro wa ramani wa jengo hilo na baada ya wiki mbili, itakuwa tayari.
Meneja Mkuu huyo, alisema tayari amewapa mafunzo ya kudhibiti majanga ya moto wafanyabiashara zaidi ya 400 wa soko hilo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo ya Rais Dk. Samia.
“Kwa kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji leo (jana), tumetoa mafunzo haya kwa wafanyabiashara wa soko letu hili ili kuhakikisha hakuna janga lolote la moto linatokea,”alisema.
Alisema shirika hilo, limeamua kuwapa mafunzo hayo kwa vitendo wafanyabiashara hao, kwa sababu itakuwa sehemu ya kudhibiti majanga ya moto, ambayo yanaweza kutokea katika soko.
KAIMU KAMANDA ZIMAMOTO
Naye, Kaimu Kamanda Mkoa wa Ilala wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Chrispin Rabiuzima, alisema mafunzo hayo ni mwendelezo wa utekelezaji wa maagizo ya Rais Samia, aliyoyatoa wakati wa ufunguzi wa soko hilo jipya.
“Tutakuwa tunawapatia mafunzo mara kwa mara wafanyabiashara hawa ili kujua namna ya kutumia vifaa vya kudhibiti majanga ya moto,” alisema.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa soko hilo, Ramadhani Kakandilo, alisema ni jambo la kupongezwa kwa uongozi wa soko hilo la kuhakikisha wafanyabiashara wanapata mafunzo ya namna ya kukabiliana na majanga ya moto.
“Mafunzo haya yatawasaidia baadhi ya wafanyabiashara kujua namna ya kutumia vifaa hivi vya kuzimia moto ambavyo vimewekwa katika soko hili, maana wengi wamekuwa wakiona katika vyombo vya habari, lakini sasa wamejifunza kwa vitendo,” alisema.




