Na LILIAN JOEL, Arusha
TANZANIA imeendelea kutikisa kiuchumi katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kutokana na kudhibiti mfumuko wa bei kwa kiwango cha asilimia 3.3 mwaka uliopita, ambao unatarajiwa kubaki asilimia 3.5 kwa robo ya mwaka wa fedha 2026/27.
Aidha, udhabiti huo, umetokana na usimamizi makini wa sera ya fedha na mifumo madhubuti ya udhibiti wa masuala ya kiuchumi nchini.
Kauli hiyo, ilitolewa jijini Arusha na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Emmanuel Tutuba, wakati akifungua mkutano wa 33 wa Kamati ya Magavana wa Benki Kuu za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (CCBG) na Kamati Ndogo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).
“Hii ni kutokana na nchi yetu kuwa na mifumo mizuri ya udhibiti wa masuala ya kiuchumi, mfumuko wa bei ulidhibitiwa kwa kutumia sera mbalimbali, ikiwemo ya fedha, kwa robo hii ya mwaka, bado mfumuko wa bei utaendelea kuwa chini kwa asilimia 3.5.
“Katika viashiria jumuishi vya makubaliano yetu katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), tumejiwekea wigo wa asilimia saba, tupo asilimia 3.5 na tutajitahidi mfumuko wa bei uwe katika kiwango cha chini zaidi,”alisema.
Kwa mujibu wa Tutuba, udhibiti huo wa mfumuko wa bei, unawezesha ununuzi wa bidhaa na huduma kwa mwaka hadi mwaka, usiwe unatofautiana.
Pia, kuendelea kuweka imani kwa wawekezaji kwa sababu, mfumuko wa bei unapokuwa chini, kuna kiwango cha ukuaji wa uchumi kinaendelea vizuri.
“Utulivu wa bei unalinda uwezo wa ununuzi wa wananchi na kuimarisha imani ya wawekezaji.
“Mfumo wa bei unapokuwa tulivu, uchumi hukua kwa kasi endelevu na uwekezaji huongezeka,” alisema.
Kuhusu mkutano huo, Tutuba alisema wataalamiu watajadili kwa kina na kuweka mipango mikakati itakayowezesha usalama na kudhibiti vihatarishi mbalimbali vinavyoweza kusababisha shughuli za kiuchumi na mabenki, zisitekelezeke ipasavyo katika ukanda wa SADC.
“Tunatarajia wataalamu watajadili kwa kina na kuweka mikakati ambayo wataiwasilisha katika Kamati ya Magavana wa Benki Kuu za SADC, tuone namna gani kwa ujumla wetu, tunaweza kuimarisha biashara na uhamilishaji wa fedha kutoka nchi moja kwenda nyingine,”alisema.
Alisisitiza kuwa, mifumo madhubuti ya malipo, ndiyo inayowezesha fedha zitoke nchi moja kwenda nyingine, kuwezesha shughuli za kiuchumi zitekelezeke ndani ya SADC na kufikia malego waliyojiwekea.
“Mifumo ya malipo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi. Ikitetereka, athari zake huanzia kwa mfanyabiashara mmoja mmoja hadi uchumi wa taifa. Ndiyo maana, tunasisitiza uimara na uendelevu wake,” alisema.
Alisema hivi sasa, kuna vihatarishi mbalimbali vinavyosababisha shughuli za kiuchumi na benki zisitekelezeke ipasavyo, ukiwemo udukuzi wa mifumo ya kifedha na masuala ya fedha katika mtandao sanjari na uwekezaji.
“Katika dunia ya sasa inayobadilika kwa kasi ya teknolojia, mifumo ya kifedha lazima iwe imara, salama na yenye uwezo wa kuhimili vihatarishi vinavyoibuka.
“Siku zote lazima mifumo ya kibenki na sekta ya fedha inatakiwa iwe endelevu kwa kufanya miamala bila kumkwamisha mtu yeyote kwa sababu, ukikwamisha miamala utasababisha hasara kwa watu na kuondoa imani kwa wale wanaofanya malipo katika shughuli zao za kiuchumi,”alisema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mifumo ya TEHAMA wa BoT, Michael Mtweve, alisema wataalamu hao, watapata fursa ya kujadili matumizi ya teknolojia ya Akili Mnemba (AI) katika kuimarisha utendaji wa benki kuu ukanda wa SADC.
Alisema pamoja na manufaa yake katika kuongeza ufanisi, teknolojia hiyo, inaweza kuleta changamoto endapo haitasimamiwa kwa umakini, hasa kukabiliana na udukuzi wa mifumo na uhalifu wa kifedha mtandaoni.
“Tunataka kupokea teknolojia mpya kwa mikakati madhubuti, kuhakikisha inaleta tija bila kuhatarisha uthabiti wa mifumo yetu ya kifedha,” alisema.
Mkutano huo unahudhuriwa na washiriki 57 kutoka nchi zote 16 za SADC na Benki Kuu ya Tanzania, imepewa nafasi ya kuwa mwenyeji wa mkutano huo kutokana na BoT kusimamia kikamilifu masuala ya ICT na usimamizi wa vihatarishi vya mabenki.




