DAKAR, Senegal
MAHAKAMA ya Usuluhishi wa Kesi Michezoni (Cas), imesema itatolea uamuzi rufaa ya timu ya taifa ya Senegal haraka iwezekanavyo baada ya miamba hiyo kupokwa ubingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON).
Senegal iliondolewa hadhi ya ubingwa wa AFCON 2025 na Shirikisho la Soka Afrika (CAF), baada ya kuvunja kanuni za mashindano kufuatia kutoka uwanjani wakati wa fainali dhidi ya Morocco.
Katika mchezo huo, Senegal ilitoka uwanjani ikigomea penalti iliyopewa Morocco dakika za mwisho kipindi cha pili kabla ya kurejea tena uwanjani na mkwaju huo ulikoswa na Brahim Diaz na mechi kwenda katika dakika 30 za nyongeza.
Katika dakika 30 za nyongeza, Senegal ilipata bao kupitia kwa Pape Gueye ambao lilidumu hadi mpira ulipomalizika (1-0) na Simba hao wa Teranga kutwaa taji hilo.
Hata hivyo, hivi karibuni CAF iliiondolea timu hiyo hadhi ya ubingwa na kuipa Morocco ushindi wa mabao 3-0 hatua ambayo imeifanya Senegal kukata rufaa Cas kupinga uamuzi huo.
Mkurugenzi Mkuu wa Cas, Matthieu Reeb alisema: “Tunaelewa kwamba timu na mashabiki wanataka kujua uamuzi wa mwisho, na tutahakikisha kwamba taratibu za usuluhishi zinafanyika haraka iwezekanavyo, wakati tukiheshima haki za pande zote katika usikilizwaji wa kiungwana,”.
Hata hivyop, taarifa hiyo haijaeleza kwamba uamuzi huo utachukua muda gani hadi kukamilika.
(BBC)




