Na NASRA KITANA
LICHA ya kusuasua katika mechi tatu zilizopita za Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu, Yanga imejivunia rekodi yake ya kutofungwa mchezo wowote katika michuano hiyo hadi sasa.
Yanga ambayo ndiyo kinara wa Ligi Kuu Bara msimu huu, hadi sasa haijapoteza mechi yoyote ikishinda mehi 11 na kutoka sare tano katika mechi 16 ilizocheza, ikivuna pointi 38.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa timu hiyo, Ally Kamwe alisema msimu huu timu yao imefanya vizuri zaidi ya msimu uliopita.
“Nawapongeza wachezaji wa timu yetu, wameonyesha juhudi kubwa katika kusaka matokeo mazuri, licha ya kukabiliwa na ratiba ngumu ya kucheza mechi mfululizo, pamoja na kukabiliwa na wachezaji wengi kuwa majeruhi,”alisema.
Kamwe alisema anajua mzunguko wa pili, utakuwa na ushindani mkubwa kwa kuwa kila timu huwa inajipanga kupata matokeo mazuri.
“Pamoja na kusuasua katika mechi tatu mfululizo tulizocheza hivi karibuni, lakini tunajivunia rekodi nzuri tulioyoiweka kwa kumaliza mzunguko wa kwanza bila ya kupoteza mchezo wowote,” alisema.
Kamwe alisema hivi sasa timu yao inaendelea na maandalizi kwa mechi zake za mzunguko wa pili na wanachohitaji ni kupata ushindi katika mechi zilizobakia.
Ofisa huyo alisema msimu huu wamefanya vizuri zaidi tofauti na ilivyokuwa katika msimu uliopita kutokana na ushirikiano mzuri uliopo kutoka kwa viongozi, wanachama, wadau na wachezaji kwa ujumla.
Yanga kesho saa 12:30 jioni itashuka dimbani kupambana na Tanzania Prisons katika Uwanja wa KMC, Dar es Salaam.




