NA FRED ALFRED
DODOMA
NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma, amesema Serikali imetenga jumla ya sh.bilioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa ukumbi mkubwa wa kisasa (Arena) pamoja na studio za kisasa za filamu nchini.
Mwinjuma aliyasema hayo bungeni jijini Dodoma, alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Makete (CCM) Festo Sanga, aliyetaka kujua ni lini mchakato wa ujenzi wa ukumbi huo utakamilika.
Akijibu hilo Mwinjuma alifafanua kuwa, serikali inaendeleza dhamira yake ya kuendelea kuimarisha sekta za sanaa, utamaduni na michezo kupitia uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya kisasa.
Mwinjuma alisema kuwa maandalizi ya utekelezaji wa mradi huo, yapo katika hatua za mwisho, huku ujenzi ukitarajiwa kuanza katika kipindi cha karibuni.
“Ujenzi wa Arena umetengewa fedha katika bajeti ya mwaka huu ambapo sh.bilioni 400 zitapatikana kutokana na mkopo wa masharti nafuu kutoka benki ya Korea na mchakato wa ujenzi utaanza hivi karibuni,”
Aliwatoa hofu wananchi na wadau wa michezo kuwa suala hilo, serikali italitekeleza na lipo katika hatua za mwisho za kuanza utekelezaji wake.




