Na EMMANUEL MOHAMED
BAADHI ya wanasiasa nchini, wameeleza faida za miaka 62 ya Muungano wa Tanganyika (Tanzania Bara) na Zanzibar.
Miongoni mwa faida ni zile za kiuchumi kwa wafanyabiashara na kuongeza wigo wa soko.
Faida nyingine ambazo zinapatikana kupitia Muungano huo ni fursa za watu wa pande zote mbili kumiliki ardhi na uhakika wa ulinzi kwa upande wa Zanzibar.
Akizungumza na UHURU, Katibu wa Kamati Maalumu ya NEC Zanzibar, Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis, alisema Muungano umewaimarisha Watanzania kiuchumi na kutumia fursa zilizopo.
“Muungano wetu umetoa fursa kwa wakazi kutoka pande zote mbili kuishi maeneo yote ya Jamhuri ya Muungano na tukumbuke kuwa, Zanzibar ardhi yake ni ndogo, hivyo wanatumia fursa hiyo kuja upande wa pili kuanzisha shughuli za kiuchumi,”alisema.
Alisema faida ya Muungano ni kwamba, Wzanzibari wanapata fursa ya kumiliki ardhi kwa shughuli za kilimo na ufugaji.
“Faida nyingine ni kutumia soko pana la kibiashara kwa Tanzania Bara, unajua idadi ya watu Tanzania Bara ni kubwa, hivi sasa wafanyabiashara wakichukua bidhaa huku na kuleta upande wa pili, wananufaika kibiashara.
“Leo ukimtazama Bakhresa, biashara yake imetanuka kutokana na Muungano, imempatia fursa ya kumiliki eneo kubwa la ardhi kwa upande wa Tanzania Bara na kuanzisha biashara nyingi,”alisema
Alisema mbali na Bakhresa, pia yupo mfanyabiashara anayeitwa Gulamali, ametumia fursa ya Muungano katika kujitanua ambayo amejikita katika shughuli za uzalishaji kupitia kilimo, ufugaji na nyingine.
“Leo hii kupitia Muungano, mtu akiona mambo magumu anakwenda upande wa pili kutafuta fursa za kiuchumi, Zanzibar hivi sasa ni kisiwa cha utalii, kuna hoteli zaidi ya 8,000, hivyo watu wanapata ajira, “alisema
JUMA ALLY KHATIB
Mwenyekiti wa ADA TADEA, Juma Ally Khatib, alisema suala la Muungano siyo tu wa kisiasa, bali ni daraja muhimu la kiuchumi.
Alisema kupitia Muungano, wafanyabiashara wa Zanzibar wanauza bidhaa zao kwa urahisi katika soko kubwa la Tanzania Bara bila vikwazo.
“Hivyo, wafanyabiashara wa Tanzania Bara wanapata fursa ya kuwekeza katika sekta za utalii, uvuvi na biashara visiwani Zanzibar,”alisema.
Pia, Mwenyekiti huyo alisisitiza kuwa, Muungano umewezesha uwekezaji wa pamoja katika bandari, usafiri wa baharini na sekta ya utalii, jambo linalochangia ukuaji wa uchumi wa pande zote.
“Muungano wetu ni hazina, thamani yake itaonekana zaidi pale tutakapowekeza katika ushirikiano wa kiuchumi na kuwajengea wananchi mazingira rafiki ya kufanya biashara,” alisema.
Muungano wa Tanganyika (Tanzania Bara) na Zanzibar, ulifanyika Aprili 26, 1964, ukiongozwa na waasisi Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Hayati Abeid Amani Karume.




