Na MWANDISHI MAALUMU
MAKAMU wa Rais, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, amesema taifa litaukumbuka mchango mkubwa alioutoa marehemu Askofu Bernadin Mfumbusa, enzi za uhai wake ukiwemo kuwa kiungo muhimu wa Kanisa Katoliki na dini zingine.
Balozi Dk. Nchimbi alisema hayo, baada ya kushiriki ibada ya kumuaga na kumwombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, Mfumbusa, iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma.
Alisema Askofu Mfumbusa alijitolea katika kuunganisha dini na madhehebu zifanye kazi kwa kuheshimiana, kushirikiana na kupendana.
Kwa mujibu wa Balozi Dk. Nchimbi, taifa litakumbuka mchango wake katika kuhamasisha elimu, kusimamia ujenzi na uendelezaji wa huduma za afya wilayani Kondoa na taifa kwa ujumla.
Makamu wa Rais alisema Askofu Mfumbusa alitoa mchango katika sekta ya mawasiliano na habari, akiwa mbobezi na mwalimu katika fani hiyo.
Nchimbi alisema Askofu Mfumbusa atakumbukwa kwa kutimiza wajibu wake kwa binadamu, kwa kutambua maisha ya kutimiza wajibu kwa Mungu.
SALAMU ZA RAIS
Pia, Balozi Dk. Nchimbi aliwasilisha salamu za pole za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, alizotoa kwa kanisa, waumini na familia na kuiombea familia nguvu na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu.
Makamu wa Rais aliwashukuru viongozi wa Kanisa Katoliki kwa malezi ya Askofu Mfumbusa ambayo yalimfanya kuwa mtume wa taifa zima.
IBADA
Ibada hiyo, iliongozwa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, Mhashamu Wilbroad Kibozi na kuhudhuriwa na maaskofu mbalimbali, mapadre, watawa, viongozi wa serikali na wananchi.



