Na AMINA KASHEBA
WAKATI mwanariadha Alphonce Simbu akivuna dola za Marekani 75,000 (zaidi ya sh. milioni 195) kwa kushika nafasi ya pili katika mbio za Boston Marathon, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amempongeza Mtanzania huyo kwa hatua hiyo kubwa.
Simbu alivuna fedha hizo baada ya kushika nafasi ya pili katika mbio hizo zilizofanyika jijini Boston, Marekani.
Katika michuano hiyo, Simbu alishinda medali ya fedha baada ya kumaliza mbio kwa muda wa saa 2:02:47.
Akiandika katika kurasa zake za mitandao ya kijamii, Rais Dk. Samia alimpongeza mwanariadha huyo kwa kushika nafasi hiyo.
“Ninatoa pongezi za dhati kwa Alphonce Simbu kwa kushika nafasi ya pili na kuweka rekodi ya Taifa katika mashindano ya kimataifa ya mbio ya Boston (Boston Marathon), kwa mara ya pili mfululizo.
“Umeendelea kuipeperusha vyema bendera ya taifa letu, ukilitangaza jina la Tanzania kimataifa katika moja ya mashindano mashuhuri zaidi duniani, na umetuletea heshima kubwa katika ulimwengu wa michezo. Mafanikio yako ni chachu ya matumaini na hamasa kwa vijana wengi,” aliandika katika ukurasa wake wa Instagram.
Dk. Samia alisema Watanzania wanajivua mwanariadha huyo kutokana na jitihada alizonazo kimataifa.
WADAU WAFUNGUKA
Mwanariadha mkongwe, Juma Ikangaa, alisema Simbu ana haki ya kufanya vizuri katika mashindano hayo kutokana na maandalizi makubwa aliyoyafanya.
Alisema mwanariadha huyo amekuwa akijituma na kufanya mazoezi kwa muda mrefu jambo ambalo lilimuongezea nguvu ya kufanya vyema katika mbio hizo.
“Tanzania tunapaswa kujivunia kwa kipaji cha Simbu kwa sababu amekuwa na jitihada kubwa za kufanya mazoezi bila kuchoka, hili ndiyo linampa ushindi katika mashindano ya kimataifa,” alisema.
Kocha, Alfredo Shahanga alisema alikuwa ana imani kwamba Simbu atafanya vizuri kutokana na maandalizi bora aliyoyafanya.
Alisema jambo ambalo amefurahia kwake ni kuvunja rekodi ya kupunguza muda wa kukimbia baada ya mwaka jana kukimbia kwa muda wa saa 2:04:38 huku mwaka huu akikimbia kwa saa 2:02:47.




