Na ATHNATH MKIRAMWENI
MHASIBU wa Kiwanda cha Kuchakata Chupa za Plastiki cha XIL LI kilichopo Mabibo wilayani Ubungo, Dar es Salaam, Eversophy Michael, amesimulia kwa kina tukio la mauaji ya mmiliki wa kiwanda hicho, Bhaozang Ge (50), ambaye ni raia wa China.
SIMULIZI
Akizungumza na UHURU jana, Eversophy alisimulia namna alivyoanza kupata hofu baada ya wafanyakazi kufika kazini na kukuta geti la kiwanda limefungwa kwa muda mrefu, huku walinzi waliokuwa zamu wakitoweka katika mazingira ya kutatanisha kabla ya mwili wa mmiliki wa kiwanda hicho, kupatikana ndani ya mtaro wa maji.
Eversophy alisema siku ya Jumamosi, wafanyakazi walifika mapema asubuhi kuendelea na shughuli za uzalishaji, lakini walishangazwa na kuchelewa kufunguliwa geti, jambo ambalo halikuwa la kawaida katika kiwanda hicho.
Alisema wafanyakazi waliendelea kugonga geti kwa muda mrefu huku wakimpigia simu Ge, lakini simu yake iliita bila kupokewa hali iliyozua taharuki miongoni mwao.
Eversophy alisema baada ya kuona hakuna anayefungua, walimpigia simu mfanyakazi mwingine raia wa China, aliyefahamika kama babu aje kufungua geti.
Alisema babu alifika, kufungua geti na wafanyakazi kuingia ndani, huku wakijiuliza walinzi walikwenda wapi.
Mhasibu huyo aliendelea kusimulia, wafanyakazi wengi walielekea moja kwa moja eneo la walinzi kuuliza sababu ya kuchelewa kufunguliwa geti, lakini hawakumkuta mtu jambo lililoongeza hofu zaidi.
Kwa mujibu wa Eversophy, muda mfupi baadaye msichana mmoja aliyekuwa akimsaidia Ge kazi za ndani aliwasili kiwandani na kuingia chumbani kwake, baada ya kuendelea kumpigia simu bila mafanikio.
ìAlipoingia ndani alikuta simu ya bosi ikiita lakini yeye mwenyewe hakuwepo,î alisema
Eversophy alisema baadaye, aliwasiliana na vituo mbalimbali vya polisi, akiamini huenda kulikuwa na vurugu usiku na watu hao kupelekwa kituoni, lakini hakupata taarifa yoyote kuhusu Ge wala walinzi hao.
Alisema walipoendelea kufuatilia walipata taarifa kutoka kwa mlinzi wa jirani, aliyedai usiku wa tukio aliwaona walinzi wawili wakitoka kiwandani majira ya tisa usiku, wakisema mwenzao alikuwa anaumwa na wanampeleka hospitali.
Mhasibu huyo alieleza kuwa, mlinzi huyo alisema mmoja wa walinzi hao alibeba begi jeusi mgongoni na kwa kuwa aliwafahamu kama walinzi wa eneo hilo hakuwazuia kuondoka.
Eversophy alisema kauli hiyo ilimfanya ahisi huenda kulikuwa na jambo baya limetokea ndani ya kiwanda hicho, ndipo alipowaagiza wafanyakazi kutawanyika kila kona ndani ya kiwanda hicho kuanza kumtafuta Ge.
Alisema wakati akiwa kituo cha polisi kuandika maelezo, alipigiwa simu na wafanyakazi waliokuwa wakitafuta ndani ya kiwanda hicho wakipiga kelele; wakisema wameuona mwili wa Ge ndani ya mtaro wa maji unaotumika kwenye mashine za kusaga na kurejeleza maji.
Eversophy alisema wakati anapewa taarifa hiyo ya mwili wa bosi wao kukutwa ndani ya mtarowa maji, tayari askari walifika kiwandani hapo kuanza uchunguzi.
Alisema baada ya mwili huo kutolewa ndani ya maji, walibaini Ge alijeruhiwa vibaya kichwani na sehemu nyingine za mwili wake huku begi alilokuwa nalo siku ya Ijumaa, halionekani.
Eversophy alisema begi hilo lilidaiwa kuwa na kiasi cha fedha kinachokadiriwa kufikia sh. milioni 10, ambazo zilikuwa za mahitaji ya kiwanda hicho.
Alisema tukio hilo limewaacha wafanyakazi wa kiwanda hicho katika simanzi kubwa, kutokana na namna Ge alivyokuwa karibu na wafanyakazi wake na jinsi kiwanda hicho kilivyokuwa kikitoa ajira kwa zaidi ya watu 200.
KUAGWA NA KUCHOMWA
Eversophy alisema kwa hivi sasa mwili wa Ge umehifadhiwa hospitali ya Jeshi Kurasini, huku familia yake akiwemo mke na watoto ikitarajiwa kuwasili kutoka China, Mei 22, mwaka huu, kushiriki taratibu za mazishi.
Alisema baada ya familia hiyo kuwasili, mwili wa Ge utaagwa katika kiwanda hicho kwa siku mbili, Jumamosi na Jumapili, kuwapa nafasi wafanyakazi, marafiki na watu mbalimbali waliokuwa karibu naye kutoa heshima zao za mwisho.
Baada ya shughuli za kuuaga mwili kukamilika, utapelekwa Makumbusho kuchomwa moto, kabla ya mabaki yake kusafirishwa kwenda China na familia yake.
Mhasibu huyo alisema Ge alikuwa mtu mwenye upendo na ushirikiano mkubwa na wafanyakazi wake, mara nyingi walikuwa wakiifanya kazi pamoja na huwezi kumjua kama ni mmkiliki wa kiwanda hicho.
Alisema katika kipindi chote alichofanya kazi naye hajawahi kushuhudia akigombana na wafanyakazi, wala kuchelewesha mishahara.
Eversophy Alisema Ge alikuwa akifanya kazi karibu na wafanyakazi wake na kiwanda hicho kilikuwa chanzo cha ajira kwa watu wengi waliokuwa wakimtegemea kwa maisha yao ya kila siku.
TAARIFA YA POLISI
Juzi, taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Kamanda wa Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro, ilieleza kufanya uchunguzi wa tukio hilo la kuuawa kwa mmiliki huyo ambaye ni raia wa China.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa tukio la kuuliwa kwa mmiliki huyo lilitokea Mei 16, mwaka huu, katika eneo la kiwanda hivyo, upelelezi wa tukio hilo unaendelea kuhakikisha watuhumiwa wanachukuliwa hatua zaidi za kisheria.



