Na MWANDISHI WETU
WAZIRI MKUU Dk. Mwigulu Nchemba, ameshiriki Mkutano wa 61 wa Mwaka wa Bodi ya Magavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) ambao umeshirikisha Wakuu wa Nchi na Serikali za Afrika na wawakilishi wao ambapo yeye amemwakilisha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Mkutano huo ambao umeanza leo (Jumanne, Mei 26, 2026) jijini Brazzaville, Jamhuri ya Kongo ulifunguliwa na Rais wa nchi hiyo, Denis Sassou-Nguesso na kuhudhuriwa na Wakuu wa Nchi na Serikali na Makamu wa Rais kutoka nchi mbalimbali.
Akizungumza kwenye ufunguzi wa mkutano huo ulioanza katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Kintele (Kintele International Conference Centre), Rais Nguesso amesema Afrika haipaswi kuishia kujivunia kuwa na utajiri wa rasilmali bali izitumie vizuri rasilimali hizo kuwanufaisha wananchi wake.
Amesema ili kuyafikia mageuzi yanayotakiwa, Afrika inahitaji kuwa na miradi ya kimkakati yenye mageuzi. “Tunahitaji kukuza masoko ya fedha na kuziwezesha taasisi za kikanda ili ziweze kukabiliana na vihatarishi vya kiuchumi kupitia ushirikiano imara. Hii itasaidia kuifanya Afrika kuwa na udhibiti wa rasilimali zake na hatimaye kuimarisha uchumi wa nchi pamoja kuboresha maisha wananchi.”
Baada ya ufunguzi, Waziri Mkuu pia alishiriki mdahalo wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu mustakabali wa ufadhili wa maendeleo barani Afrika (Presidential High-Level Panel on Africa’s Development Financing) ambao uliwashirikisha Rais wa Jamhuri ya Congo, Denis Sassou Nguesso, Rais wa Jamhuri ya Afrika ya Kati, Faustin Archange Touadéra Rais wa Jamhuri ya Gabon, Brice Clotaire Oligui Nguema na Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Sidi Ould Tah.
Vilevile, Waziri Mkuu alishiriki kwenye mdahalo wa uzinduzi wa taarifa ya African Economic Outlook 2026 na mkutano wa wadau wa maendeleo kuhusu ufadhili wa Mpango wa Uwekezaji wa Blue Fund for the Congo Basin.




