Na MWANDISHI WETU
KIKOSI cha Yanga kimeukaribia ubingwa wa michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara, kufuatia kupata ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Azam FC, katika mchezo uliochezwa Uwanja wa New Amaan, Complex, Zanzibar.
Watani wao wa jadi, Simba nao waliendeleza kazi kazi,baada ya kuitandika Mtibwa Sugar mabao 3-0 katika mechi iliyofanyika Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro.
Baada ya ushindi huo, Yanga inaendelea kusalia kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi 69 huku Simba ikishika nafasi ya pili kwa pointi 67, Azam FC ipo nafasi ya tatu kwa alama 58 huku timu zote zikishuka dimbani mara 28 na kubakisha mechi mbili kumaliza msimu huu.
Yanga imebakiwa na mechi mbili dhidi ya timu za TRA United na JKT Tanzania huku Simba ikisalia na michezo dhidi ya Singida Black Stars na KMC, wakati Azam FC ikipepetana dhidi ya Coastal Union na Dodoma Jiji.
Magoli ya Yanga yalifungwa na wachezaji wake, Ibrahim Bacca dakika ya 41, Laurindo Dilson ‘Depu’ penalti (71) na Pacome Zouzoua (80).
Mabao ya Simba katika mchezo wa jana, yalipachikwa wavuni na Rushine De Reuck kwa penalti dakika ya tisa, Selemani Mwalimu (77) na Anicet Oura (90).
Katika mechi ya Yanga na Azam FC, mchezo ulikuwa wa kasi na kushambuliana kwa kila timu ikitaka ushindi na kujiwekea masingira mazuri.
Dakika ya 35, Yanga walipata nafasi ambapo Prince Dube alishindwa kuitumia kutokana na shuti lake kupaa juu ya lango.
Dakika ya 37, Azam ilijibu shambulizi ambapo mchezaji wake Idd Nado alifumua shuti lililotoka nje ya lango.
Katika dakika ya 41, Bacca aliwainua katika viti mashabiki wa Yanga baada ya kufunga bao la kuongoza akiunganisha kwa kichwa pasi iliyotoka kwa Prince Dube.
Dakika ya 51, Azam nusura wapate bao kufuatia Feisal Salum ‘Fei Toto’ kugonga kichwa mpira ukaishia mikononi mwa kipa wa Yanga, Djigui Diarra pasi ya mwisho ilitoka kwa Nado.
Katika dakika ya 71, Yanga walipata bao la pili likiwekwa kimiani na Depu kwa mkwaju wa penalti baada ya kuchezewa madhambi na Twalibu Nuru katika eneo la hatari.
Wakitandaza kandanda safi huku wakigongeana pasi fupi fupi, Yanga walipata bao la tatu likiwekwa kimiani na Pacome dakika ya 80 baada ya kutokea piga nikupige langoni mwa Azam.
Hadi mchezo unamalizika, Yanga waliibuka na ushindi wa mabao 3-0.
Matokeo ya mechi zingine, Singida Black Stars ilishinda mabao 3-1 mbele ya Tanzania Prisons, Namungo FC iliichapa KMC mabao 3-2 na Mbeya City ikiifunga 2-0 Pamba Jiji.
Pia Mashujaa FC ilishinda bao 1-0 dhidi ya Fountain Gate, TRA United ikitoka sare ya 1-1 mbele ya Coastal Union huku Dodoma Jiji ikisuluhu dhidi ya JKT Tanzania.
Baada ya mchezo huo, Kocha wa Yanga, Abdihamid Moallin alisema amefurahi kupata ushindi na kujiweka katika nafasi nzuri ya kutangaza ubingwa kwa mara nyingine msimu huu.
Kocha wa Azam, Florent Ibenge alisema anawapongeza Yanga kwa kupata ushindi japokuwa wao walipata nafasi nyingi na kushindwa kuzitumia kupachika mabao.
Yanga: Djigui Diarra, Bakari Mwamnyeto, Ibrahim Bacca, Maxi Nzengeli, Pacome Zouzoua, Mohamed Hussein, Allan Okello, Prince Dube, Laurindo Dilson, Koussi Yao na Duke Abuya.
Azam FC: Zuberi Foba, Lusajo Mwaikenda,Twalibu Nuru, Lameck Lawi, Paschal Msindo, Sadio Kanoute, Himid Mao, Iddi Selemani, Jean Ngita, Feisal Salum na Zidane Sereri.




