Na AMINA KASHEBA
NI dhahiri kuwa mechi ya Yanga dhidi ya Azam FC bado haijaisha, kwani timu hizo bado zina kibarua kingine zitakapopambana katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Yanga na Azam FC zitapepetana tena kesho, katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, utakaopigwa Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.
Vigogo hivyo vitapambana ikiwa ni siku tatu baada ya Yanga kukubali kipigo cha mabao 3-2, katika mchezo wa nusu fainali ya Kombe la Shirikisho (FA), iliyochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita, katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Kipigo cha Yanga
Macho na masikio kutoka kwa mashabiki wa timu hizo, wadau wa soka ni kuona kama Yanga inayotetea taji la Ligi Kuu itakubali tena kichapo au itashinda mechi hiyo muhimu dhidi ya Azam na kuendelea kujiweka katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa.
Katika msimamo wa ligi, Yanga inaongoza ikiwa na pointi 66 huku mtani wake wa jadi, Simba, ikiwa na alama 64, zikitofautiana kwa alama mbili.
Kama Yanga itapoteza mchezo dhidi ya Azam huku Simba ikashinda mchezo ujao dhidi ya Mtibwa Sugar, kuna uwezekano wa kupoteza ubingwa.
Lakini kama Yanga itashinda huku Simba ikipoteza, Yanga itakuwa bingwa, kutokana na hali hiyo, pambano kati ya Azam na Yanga ni la kukata na soka na lazima limalizwe kwa ushindi mnono.
KAULI YA MOALIN
Kocha wa Yanga, Moalin alisema mechi dhidi ya Azam ni jaribio lingine gumu ambalo linapaswa kujibiwa kwa kupata ushindi na si vinginevyo.
Molanin alisema pamoja na kupoteza mechi ya FA, timu yake si dhaifu kama inavyoelezwa na mashabiki ambao hawaitakii Yanga mema.
Alisema anaamini kuwa makosa yaliyojitokeza katika pambano lililopita hayawezi kujirudia na kikosi chake kipo tayari kujibu mapigo.
“Mchezo uliopita ulikuwa na ushindani mkubwa, yaliyopita yanapaswa kusahaulika na kujipanga kwa kile kilichopo mbele yetu,” alisema Moalin.
“Wachezaji wangu walipata nafasi kadhaa za kufunga, lakini walishindwa kuzitumia vizuri kupata bao, hilo tatizo limechangia kufungwa na Azam FC, “ aliongeza.
Meneja Habari na Mawasiliano wa Yanga, Ally Kamwe, alisema haikuwa bahati kwa Yanga kucheza fainali za msimu huu hivyo nguvu zote zimeelekezwa katika mechi zilizobaki za ligi.
“Timu ilicheza vizuri na kutengeneza nafasi nyingi za kufunga, ilirudisha mabao ya utangulizi lakini bahati haikuwa upande wetu,” aliongeza Kamwe.
TAMBO ZA IBENGE
Kocha wa Azam FC, Florent Ibenge, alisema ni muda wa kukiongoza tena kikosi chake kupata matokeo mazuri dhidi ya Yanga.
Ibenge alisema wachezaji wake wapo katika hali nzuri na jana waliendelea na mazoezi kujiwinda na mechi nyingine na Yanga.
Nahodha wa Azam, Himid Mao, alisema timu yao ipo tayari kujiuliza tena kwa Yanga.
Mao aliwapongeza wachezaji wenzake kwa kufanya vyema katika mechi iliyopita na kuahidi kutakata tena mbele ya Yanga katika mchezo wa kesho.



