Na NASRA KITANA
WAKATI Ligi Kuu Tanzania Bara msimu 2025/26 ukiwa umemalizika, uongozi wa klabu ya Azam FC umetangaza bajeti ya sh.bilioni nane kwa ajili ya kusuka kikosi chao cha msimu ujao.
Katika msimu uliomalizika hivi karibuni, Azam haikuambulia chochote baada ya kumaliza nafasi ya tatu katika msimamo wa ligi ikiwa na pointi 64 na kucheza fainali ya Kombe la Shirikisho(FA) na kuwa mshindi wa pili baada ya kufungwa na Simba bao 1-0.
Kwa mujibu wa kiongozi mmoja wa timu hiyo, alisema tayari wametenga bajeti hiyo kuhakikisha wanafanya usajili wa viwango vya juu.
Alisema tayari Kocha Mkuu wa timu hiyo, Florent Ibenge ametoa ripoti ya wachezaji ambao wataachwa ndani ya kikosi hicho na wale ambao wataingia kuongeza nguvu msimu ujao.
“Msimu ujao tunataka uwe msimu wa tofauti, tumetenga fedha hiyo kwa ajili ya kuleta wachezaji wapya wenye viwango vikubwa, tutafanya marekebisho ya baadhi ya wachezaji ambao mwalimu anawahitaji na tutawaondoa wale ambao hawakuwa na mchango katika timu,” alisema kiongozi huyo ambaye hakutaka jina lake liwekwe hadharani.
Alipoulizwa jana na mwandishi wa habari hii,msemaji wa timu hiyo, Hasheem Ibwe alisema kama timu wametenga fedha nyingi kuhakikisha wanafanya usajili mzuri.
Alisema hawakuwa na msimu mzuri, lakini hawatakubali msimu ujao kuwa wanyonge tena.
“Tumetenga bajeti kubwa ya kuhakikisha tunamsajili mchezaji yeyote ambaye tunamuhitaji, msimu ujao tunataka uwe msimu bora na kufikia malengo ambayo tumejiwekea,” alisema Ibwe.
Ofisa habari huyo aliwataka mashabiki na wapenzi wa timu hiyo kuendelea kuwapa sapoti ya kutosha wachezaji wao, wafanye vizuri.
Hata hivyo, tetesi zinaeleza kuwa Azam FC inatarajiwa kuwaacha wachezaji zaidi ya wanane ili kusuka kikosi kipya.




