Na NASRA KITANA
BAADA ya kuishia hatua ya robo fainali katika Fainali za Mataifa ya Afrika kwa Wachezaji wa Ligi za Ndani (CHAN 2024), timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, imeanza kufanya maandalizi ya kampeni ya kufuzu Kombe la Dunia.
Stars inatarajiwa kucheza mchezo wa kwanza ugenini dhidi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), utakaopigwa Septemba 5, mwaka huu.
Baada ya mchezo huo, Stars itarudi dimbani kupambana na Niger ambapo pambano hilo limepangwa kufanyika Septemba 9, mwaka huu katika Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Cliford Ndimbo amesema upande wa benchi la ufundi wanajiandaa kutangaza kikosi hicho.
Ndimbo amesema Kocha, Hemed Suleiman ‘Morocco‘ anatarajia kutangaza kikosi bora ambacho kitaenda kupambana kusaka alama sita katika mechi hizo mbili.
“Tumeanza maandalizi kwa mechi hizo mbili ambazo ni muhimu kwetu kocha anatarajia kutangaza kikosi kesho.
“Tuna imani kubwa kwamba timu yetu itafanya vizuri katika mechi hizo na kuipeperusha vyema bendera ya nchi,” alisema ofisa huyo.
Hata hivyo, Ndimbo aliipongeza Taifa Stars kwa kufika hatua ya robo fainali ya mashindano ya CHAN 2024 kwani ni hatua kubwa na wameweka historia ya aina yake.
Amesema kuwa ana imani msimu ujao wa katika mashindano hayo, Stars itafika mbali zaidi na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania.
“Ukweli nachukua fursa hii kuwapongeza wachezaji wa Taifa Stars kwa kujituma na kufika hatua ya robo fainali ya CHAN 2024, tumepata uzoefu mkubwa na nina imani kuwa wataenda kufanya vizuri zaidi katika mechi zinazofuata,” amesema.
Ofisa huyo alisema anaishukuru serikali kwa ushirikiano mkubwa waliouonesha kuanzia mashindano hayo yalivyoanza hadi kufikia tamati.




