Na MUSSA YUSUPH,
SINGIDA
YAJAYO yanafurahisha! hiyo ndiyo kauli ya Mgombea Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan, aliyoitoa akiwaahidi Watanzania, endapo akipewa ridhaa ya kuliongoza taifa kwa kipindi kingine, Tanzania itakuwa nchi yenye neema zaidi.
Ahadi hiyo, ameitoka katika mikutano yake ya kampeni, iliyofanyika wilayani Bahi (Dodoma) Manyoni, Ikungi na Singida Mjini mkoani Singida, Uwanja wa Bombadia.
Katika mikutano hiyo iliyohudhuriwa na maelfu ya wananchi, Dk. Samia, alisisitiza kuwa, hiyo ndiyo moja ya dhamira iliyomfanya kuomba ridhaa ya kuliongoza Taifa.
Akizungumza katika mkutano wa kampeni za Uchaguzi Mkuu uliofanyika Uwanja wa Bombadia, Singida Mjini, Dk. Samia, alisema uwekezaji unafanyika nchi nzima kujali utu wa mtu.
“CCM inaweka ilani yake kuweka uwekezaji kwa kutumia fedha nyingi kama zinavyotajwa, kujali na kuinua utu wa mtu. Tunataka kila Mtanzania tujali utu wake.
“Tujali afya yake, tujali elimu yake, tujali usalama wake, tujali kila kitu kinachomgusa Mtanzania hata uchumi na ustawi wake,”alisema.
Alisema yote yanayofanyika ni katika kujali utu wa Mtanzania na kuwaomba Watanzania kuipa ridhaa CCM ikafanye makubwa zaidi yanayomjali Mtanzania.
Akizungumzia miradi ya maendeleo katika mkoa huo, alisema CCM iliahidi kufikisha umeme katika vijiji vyote 441 mkoani hapa kazi ambayo imekamilika.
Alieleza kuwa, serikali inaendelea kusambaza umeme katika vitongoji kazi ambayo inatarajiwa kukamilishwa ndani ya miaka mitano ijayo.
Katika kilimo, alisema mkoa huo, unasifika kwa kilimo na kulikuwa na skimu tatu za umwagiliaji, hata hivyo, kulikuwa na uhitaji wa skimu zingine zaidi.
“Tumeleta zaidi ya sh. bilioni 81.1, kukarabati na kujenga upya skimu za umwagiliaji zilizonufaisha wakulima 12,167 katika vijiji 67 vya Mkoa wa Singida.
“Tunapoendelea mbele mkitupa ridhaa, tutaendelea kuwezesha upatikanaji ruzuku ya mbolea na kuanzisha vituo vya ukodishaji zana za kilimo kwa bei nafuu,” alibainisha.
Vilevile, alisema serikali imeendelea kuboresha mifumo ya kuuza mazao, lengo kuu ni kuhakikisha usafirishaji mazao na mkulima moja kwa moja na kuondoa madalali waliokuwa wakimnyonya mkulima.
Alieleza kuwa, mkoa huo, mwaka jana ulianzishwa mfumo wa stakabadhi ghalani kwa mazao kupitia soko la mtandao kwa mazao ya dengu, mbaazi, choroko na ufuta kwa maeneo yanayozalisha ufuta.
“Hatua hiyo ya kubadili mifumo, imesaidia kuongeza uwazi kwa mfano mwaka jana, wastani wa bei ya mkulima ilifika asilimia 70 ya bei ya soko la dunia alipata mkulima hapa Tanzania,” alisema.
Aliongeza: “Nafahamu zipo changamoto za wanunuzi kuchelewesha malipo badala ya kulipa ndani ya saa 48, wanachukua siku tatu hadi nne, nataka niwaambie tayari serikali imekwishachukua hatua.”
Alizitaja hatua hizo ni kuwafutia leseni wanaohujumu mfumo huo, wakiwemo wanaoweka uchafu katika mazao na wanaonunua nje ya mfumo.
“Hawatapatiwa tena kibali cha kuuza nje, yaani hao ndiyo wamejiondoa katika soko, hapa kuna ombi la mgombea ubunge wa Ilongelo (Haidary Gulamali) kwamba dengu zipo ghalani unatuambiaje.
“Nataka kusema kwamba, tunahangaika kutafuta masoko, wakulima wenye mazao tulieni, tutatoa vibali vya kusafirisha nje kwa wale ambao tutawapa vibali, bado tunahangaika kutafuta soko la dengu na mbaazi,” alisisitiza.
Alisema serikali ipo katika mazungumzo na serikali ya India na mazungumzo yamefikia pazuri na bei haitashuka chini ya soko la dunia.
Dk. Samia alisema mwaka huu uzalishaji umekuwa mkubwa duniani hata nchini uzalishaji wa mbaazi na dengu umeongezeka.
“Kwa ujumla bei ya dunia imeshuka lakini tupo kwenye mazungumzo. Pamoja na hayo bado bei ya mnadani kwenye stakabadhi ghalani ni bora zaidi kuliko bei ya madalali. Hatutashuka chini ya asilimia 60 ya bei ya soko la dunia,” alisisitiza.
Aliwataka wafanyabiashara kuheshimu mifumo ambayo serikali imeamua kwenda nayo huku akiwahakikishia wakulima kwamba, serikali itaendelea kuboresha mifumo ya kuuza mazao.
Vilevile, alisema mfumo wa ushirika utapitiwa upya ili uwe wenye tija zaidi kwa mazao hayo.
Kuhusu kituo cha kupoza umeme, alisema kuna mradi wa gridi imara ambao utaanza kutekelezwa mwakani.
“Mradi huu, tumeuweka katika programu hiyo na utakwenda kutekelezwa. Kuhusu mradi wa kuzalisha umeme kwa nguvu ya jua wenye thamani ya dola milioni 80 tayari tumekamilisha upembuzi yakinifu.
“Majadiliano yanaendelea kumpata mwekezaji kwa kushirikiana na serikali kupitia utaratibu wa ubia na sekta binafsi ili mradi kuanze kutekelezwa,” alisisitiza.
IKUNGI NEEMA TUPU
Katika hatua nyingine, akizungumza na wananchi wilayani Ikungi, Dk. Samia, aliahidi ujenzi wa vituo 10 vya afya wilayani hapo kuongeza upatikanaji huduma za afya.
“Tumejipanga kujenga vituo vingine 10 vya afya ndani ya wilaya hii. Vituo vitano ni kwa Ikungi Mashariki ambavyo vitakwenda katika maeneo ya Siuyu, Ligwa, Mkiwa, Isuna na Mang’onyi.
“Vituo vingine vitano kwa Ikungi Magharibi ambavyo vitakwenda Puma, Muntiri, Minyuge, Igongwe na Mwaru,” alisisitiza.
Kuhusu umeme, alisema vijiji vyote 101, vimefikishiwa nishati hiyo huku kazi ya kuendelea kuisambaza ngazi ya vitongoji ikiendelea.
“Mbele tunapokwenda mkitupa ridhaa tutakwenda kukamilisha kazi zote ili Tanzania yote ipate nishati ya umeme,” alisisitiza.
KAULI YA MACHIFU
Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Machifu Tanzania, ambaye ni Chifu wa Mkoa wa Singida, Chifu Mugheni Senge, alisema machifu wanamuunga mkono Dk. Samia.
“Tunaona Tanzania inavyomeremeta, sisi machifu tunapata faraja kubwa kuwa na kiongozi kama wewe,” alisisitiza.
Aliahidi kura za kutosha kutoka kwa machifu na wananchi wa Mkoa wa Singida.




