Na MUSSA YUSUPH,
Singida
MGOMBEA Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema serikali imeendelea kuboresha mifumo ya kuuza mazao ya wakulima.
Amesema lengo kuu ni kuhakikisha usafirishaji mazao na kuondoa madalali waliokuwa wakimnyonya mkulima.
Dk. Samia, aliyasema hayo katika mkutano wake wa kampeni uliofanyika juzi uwanja wa Bombadia mkoani Singida.
“Hatua hiyo ya kubadili mifumo, imesaidia kuongeza uwazi, kwa mfano mwaka jana, wastani wa bei ya mkulima, ilifika asilimia 70 ya bei ya soko la dunia, alipata mkulima hapa Tanzania,” alisema.
Aliongeza: “Nafahamu zipo changamoto za wanunuzi kuchelewesha malipo badala ya kulipa ndani ya saa 48, wanachukua siku tatu hadi nne, nataka niwaambie tayari serikali imechukua hatua.”
Alizitaja hatua hizo ni kuwafutia leseni wanaohujumu mfumo huo, ikiwemo wanaoweka uchafu katika mazao na wanaonunua nje ya mfumo.
“Hawatapatiwa tena kibali cha kuuza nje, yaani hao ndiyo wamejiondoa katika soko ila hapa kuna ombi la mgombea ubunge wa Ilongelo (Haidary Gulamali) kwamba, dengu zipo ghalani unatuambiaje.
“Nataka kusema kwamba, tunahangaika kutafuta masoko, wakulima wenye mazao tulieni, tutatoa vibali vya kusafirisha nje kwa wale ambao tutawapa vibali, lakini bado tunahangaika kutafuta soko la dengu na mbaazi,” alisisitiza.
Alisema serikali ipo katika mazungumzo, yamefikia pazuri, hivyo bei haitashuka chini ya soko la dunia.
Dk. Samia, alisema mwaka huu, uzalishaji umekuwa mkubwa duniani, hata nchini uzalishaji wa mbaazi na dengu umeongezeka.
“Kwa ujumla, bei ya dunia imeshuka, lakini tupo katika mazungumzo.
“Pamoja na hayo, bado bei ya mnadani katika stakabadhi ghalani ni bora zaidi kuliko bei ya madalali. Hatutashuka chini ya asilimia 60 ya bei ya soko la dunia,” alisisitiza.
Aliwataka wafanyabiashara kuheshimu mifumo ambayo serikali imeamua kwenda nayo, huku akiwahakikishia wakulima kwamba, serikali itaendelea kuboresha mifumo ya kuuza mazao.
Vilevile, alisema mfumo wa ushirika utapitiwa upya ili uwe wenye tija zaidi kwa mazao hayo.




