Na MUSSA YUSUPH,
Dodoma
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ametangaza Baraza la Mawaziri lililosheheni sura mpya, wengi wao wakiwa vijana huku likiwa imebeba mabadiliko katika muundo wa baadhi ya wizara zilizokuwa awali.
Katika baraza hilo jipya lililojumisha wizara 27, Rais Dk. Samia, amesema mabadiliko ya kimuundo, yamefanyika kwa iliyokuwa Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, ambayo sasa itaitwa Wizara ya Kazi, Ajira na Mahusiano.
Sura mpya zilizochomoza katika baraza hilo ni Makatibu wakuu wastaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Bashiru Ali na Daniel Chongolo, Mshauri wa Masuala ya Vijana na Biashara, Joel Nanauka, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Profesa Riziki Shemdoe na aliyekuwa Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma, Caspar Mmuya.
Pia, Dk. Samia, ametimiza ahadi yake aliyoitoa wakati alipohutubia Bunge Novemba 14 mwaka huu ya kuunda wizara maalumu ya vijana, itakayoshughulikia changamoto na mengine muhimu yanayogusa kundi hilo.
Hata hivyo, katika uteuzi huo, waliokuwa baadhi ya mawaziri katika kipindi kilichopita, wamewekwa pembeni ambao ni aliyekuwa Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, aliyekuwa Waziri wa Afya, Jenista Mhagama, aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Selemani Jafo.
Wengine ni Innocent Bashugwa (Mambo ya Ndani), Pindi Chana (Maliasili na Utalii) na Dk. Damas Ndumbaro, aliyekuwa Waziri wa Katiba na Sheria.
Akizungumza alipokuwa akitangaza baraza hilo jipya tangu kukamilika kwa uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 29 mwaka huu jijini hapa, Rais Dk. Samia, alisema mawaziri wapya wateule, wataapishwa leo, Ikulu ya Chamwino nje kidogo ya Jiji la Dodoma.
“Tumeitana tuzungumze mustakabali wa serikali na taifa letu, juzi (Ijumaa) nikiwa ninazungumza na Bunge, nilisema sitochukua muda mrefu nitaunda Baraza la Mawaziri.
“Sasa ujio wangu hapa ni kuwataja wale watakaotusaidia katika kazi hizo za mawaziri na naibu mawaziri.
“Lakini niseme kwa ujumla kwamba, wizara zetu tumeona umuhimu kuona vijana kuwa na wizara kamili ambayo itasimama nayo.
“Wizara hii, itakuwa chini ya Ofisi ya Rais, lakini vilevile tumefanya mabadiliko kidogo katika Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana,” alieleza.
Alisema baada ya kuundwa Wizara ya Vijana, hivyo ameona umuhimu kuunda Wizara ya Kazi, Ajira na Mahusiano.
“Maana yake ni kwamba, atakayeshika sehemu hii ya mahusiano, atakuwa na kazi kubwa ya kufanya mazungumzo na makundi na wahusika mbalimbali nchini, kujenga mahusiano mazuri, ambayo nayo itakuwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu,” alisisitiza Rais Dk. Samia.
MAWAZIRI WALIOTEULIWA
Rais Dk. Samia, alisema Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Waziri wake ni Ridhiwani Kikwete huku Naibu Waziri akiwa Regina Kwarai.
Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, itaongozwa na Profesa Kitila Mkumbo na Naibu Waziri ni Pius Chaya.
Ofisi ya Maendeleo ya Vijana, Rais Samia amemteua Joel Nanauka kuongoza wizara hiyo, ambayo haitakuwa na naibu waziri kwa sababu, itakuwa chini ya Ofisi ya Rais, hivyo atakuwa na wasaidizi wengi.
Kadhalika, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Waziri ni Mhandisi Hamad Yusuph Masauni huku Naibu Waziri akiwa Dk. Festo Ndugange.
Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, William Lukuvi na Naibu Waziri ni Ummy Nderiyananga.
Rais Dk. Samia, alitangaza kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Waziri ni Clement Sangu, Naibu Waziri ni Rahma Kisuo, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), ambapo sasa itakuwa chini ya Waziri Mkuu, badala ya Ofisi ya Rais.
Alisema katika wizara hiyo, Waziri ni Profesa Riziki Shemdoe, Naibu Waziri ni Ruben Kwagila (Elimu) na Dk. Jafar Seif (Afya) huku Balozi Mussa Omary, ameteuliwa kuwa Waziri wa Fedha, akisaidiwa na naibu mawaziri wawili.
Naibu mawaziri hao ni Lurent Rusetula na Mshamu Ali Munde, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, itaongozwa na Balozi Mahmud Thabit Kombo na naibu mawaziri wake ni Dk. Ngwalu Maghembe na James Ole Milya.
“Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Waziri ni Boniface Simbachawene na Naibu Waziri ni Dennis Londo, Wizara ya Kilimo, itaongozwa na Daniel Chongolo na Naibu Waziri ni David Silinde.
“Wizara ya Maji imebaki kama ilivyo, Jumaa Aweso ni Waziri na Naibu Waziri ni Kundo Mathew.
“Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Waziri ni Raymond Nyansaho, Wizara ya Ujenzi, Waziri ni Abdallah Ulega na Naibu Waziri ni Mhandisi Godfrey Kasekenya,” alieleza.
Kwa upande wa Wizara ya Uchukuzi, alisema Waziri ni Profesa Makame Mbarawa na Naibu Waziri ni David Kihenzile, Wizara ya Viwanda na Biashara, itaongozwa na Judith Kapinga huku Naibu Waziri ni Patrobas Katambi.
Pia, alisema Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, itaongozwa na Angela Kairuki na Naibu Waziri ni Sweetbert Mkama, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalumu, itaongozwa na Dk. Doroth Gwajima na Naibu Waziri ni Maryprisca Mahundi.
Alieleza kuwa, Wizara ya Afya itaongozwa na Mohammed Mchengerwa, Naibu Waziri ni Frolence Samizi, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, itaongozwa na Profesa Adolf Mkenda huku Naibu Waziri akiwa ni Wanu Hafidh Ameir.
Rais Dk. Samia, alisema Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, itaongozwa na Dk. Leonard Akwilapo huku Naibu Waziri akiwa ni Casper Mmuya, Wizara ya Maliasili na Utalii, itaongozwa na Dk. Ashatu Kijaji na Naibu Waziri ni Hamad Hassan Chande.
Alisema Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Waziri ni Profesa Paramagamba Kabudi huku naibu mawaziri ni Hamis Mwinjuma (Mwana FA) na Paul Makonda.
Dk. Samia, alieleza kuwa, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, itaongozwa na Balozi Dk. Bashiru Ali, Naibu Waziri ni Ngwasi Kamani, Wizara ya Madini, itaongozwa na Antony Mavunde huku Naibu wake, akiwa Dk. Steven Kiruswa.
Alieleza kuwa, Wizara ya Nishati, itaongozwa na Deogratius Ndejembi, Naibu Waziri ni Salome Makamba, Wizara ya Katiba na Sheria, itaongozwa na Juma Homera na Naibu Waziri ni Zainab Katimba.
WACHAMBUZI
Mchambuzi wa masuala ya siasa, Doto Yotham, alipongeza uteuzi wa baraza jipya la mawaziri akisema limeleta mwelekeo na matarajio mapya hasa vijana, fursa iliyokuwa ikisubiriwa muda mrefu.
Alisema katika baraza lililopita, mawaziri wenye umri chini ya miaka 50, walikuwa asilimia 48, lakini baraza jipya, idadi imeongezeka hadi zaidi ya asilimia 60 au 70.
Alisema ongezeko hilo, linaashiria nguvu mpya serikalini, hususan katika sekta kama michezo, ambako vijana wamekuwa wakisubiri mabadiliko yatakayofanya michezo kuwa ajira halisi.
Yotham alisema viongozi vijana wenye maono, wataisukuma mbele sekta hiyo na kuongeza tija katika uchumi wa vijana.
Akizungumzia uteuzi wa George Simbachawene kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, alisema wizara hiyo ni nyeti, inahitaji mtu makini, mtulivu na mwenye uamuzi, sifa ambazo anazo.
Alisema uteuzi wa Dk. Dorothy Gwajima kuongoza Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalumu ni mzuri kwa sababu, amekuwa mstari wa mbele kushirikiana na jamii.
Pia, alisema uteuzi wa kijana kuongoza wizara inayoshughulikia masuala ya vijana ni hatua muhimu, kwa kuwa, vijana kwa muda mrefu, wamekuwa wakipaza sauti wakitaka jukwaa lao huru la kuwasilisha mawazo na changamoto zao bila kuingiliwa.
Alisema uongozi huo, unatarajiwa kuunganisha vijana walioko vyuoni, mitaani, shambani, walio na chama na wasiokuwa na chama.
Alisema changamoto kubwa inayoikabili serikali ni ajira kwa vijana, jambo ambalo hata Rais Dk. Samia, amelifafanua vizuri.
Alishauri ushirikiano wa karibu kati ya wizara ya elimu na wizara ya vijana ili mfumo wa elimu ubadilike kuwa ile inayoandaa kijana kufanya kazi.
Mwenyekiti wa Umoja wa Jukwaa la Vijana Tanzania (UWAVITA), George Shiganga, alimpongeza Rais Dk. Samia kwa uteuzi mpya wa Baraza la Mawaziri, ambalo kwa kiasi kikubwa, litaleta mafanikio ya maendeleo.
Akizungumza na gazeti hili, Shiganga alisema baraza jipya, limekuja na sura mpya ambazo zinaonekana zitakwenda kasi ya maendeleo.
“Nampongeza Rais Dk. Samia kwa uteuzi wake huo, ambao tuna uhakika Watanznaia utatufikisha tunapohitaji hasa kwenye suala la maendeleo,”alisema.
“Nimeona Baraza hili likiwa na mawaziri vijana, ambao kwa upande wetu, tunajua watatufikisha tunapohitaji hasa katika suala la ajira, mikopo na maendeleo ya vijana,”alisema.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA), Dk. Philip Daninga, alimpongeza Rais Dk. Samia kuwachanganya viongozi wapya na zamani.
Alisema hatua hiyo, itawasaidia viongozi wapya walioteuliwa, kupata uzoefu kutoka kwa viongozi wa zamani, ambao bado wapo katika nafasi za uongozi.
Kwa mujibu wa Dk. Daninga, uteuzi huo wa mawaziri, utasaidia serikali kupata nguvu ya kutosha ya utendaji kazi mzuri.
“Niwaombe viongozi waliochaguliwa kufanya kazi kwa bidii, kuwa wabunifu bila kusahau kumuunga mkono Rais Dk. Samia kwa kasi yake anayoifanya ya kuiletea nchi maendeleo ,”alisema.




