Na MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba, ametoa siku 10 kwa watendaji wa taasisi zinazohusika na usafiri wa mwendokasi jijini Dar es Salaam, kuainisha maeneo ya kufanyiwa kazi haraka, kurejesha hali ya mpito wakati serikali ikitafuta suluhisho la kudumu.
“Wizara ya Ujenzi, TANROADS, DART, UDART, OWM-TAMISEMI, TANESCO na wadau wengine, kaeni kuanzia leo (jana), husisheni mabenki, rejesheni intaneti, umeme, mageti ya kukatia tiketi ili turejeshe hali ya mpito wakati tukitafuta suluhisho la kudumu,” alisema.
Waziri Mkuu, alitoa maagizo hayo, akizungumza na wakazi wa Dar es Salaam katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Mbezi, wilayani Ubungo, jijini humo.
Alikuwa katika ziara ya siku moja, kukagua miundombinu iliyoharibiwa na vurugu zilizotokea Oktoba 29, mwaka huu na kutoa pole kwa wakazi walioathiriwa na vurugu hizo.
“Nimekuja kutoa pole kwa Watanzania walioathiriwa na tukio hili. Ninaungana na Mheshimiwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kutoa pole kwa wote walioathirika na vurugu zilizotokea Oktoba 29, 2025.”
“Tuangalie upya hatua zetu tunazozichukua. Mheshimiwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, aliunda Tume kuliangalia jambo hili, ninawaomba tumuunge mkono Mheshimiwa Rais na wajumbe wa Tume iliyoundwa kuchunguza undani wa tukio la vurugu zilizotokea, tujue namna lilivyofanyika na hatua stahiki zitakazochukuliwa,” alisema.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alisema Rais Dk. Samia, ameelekeza hakutakuwa na maadhimisho ya Sherehe za Uhuru za Desemba 9, 2025, badala yake, fedha ambazo zilipaswa kutumika kwenye sherehe hizo, zitumike kurekebisha miundombinu iliyoharibika kutokana na vurugu zilizotokea Oktoba 29, mwaka huu.
Alielekeza viongozi wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) na sekta zinazohusika, wakae na kuratibu fedha hizo, ili jambo hilo, lifanyike haraka ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais Dk. Samia.
Wakati huohuo, Rais Dk. Samia, ametoa msamaha kwa taasisi za kidini zenye changamoto na kuielekeza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, ilifungulie Kanisa la Ufufuo na Uzima na taasisi nyingine za kidini, lipewe miezi sita ya uangalizi katika kuzingatia miiko, masharti na sheria za uendeshwaji wake.
“Waziri wa Mambo ya Ndani, baada ya hapa fuatilia utaratibu mzuri, ziandikie upya taasisi za kidini, miiko yao na masharti ya uandikishaji na zile ambazo zilikuwa na shida ziweke kwenye uangalizi wa miezi sita, ipo taasisi ya Ufufuo na Uzima, nenda kaifungulie. Ifungulie, wape masharti ya uangalizi ndani ya miezi sita. Ziandikie taasisi zote za kidini kuzikumbusha miiko na mipaka ya ufanyaji kazi, sawasawa na sheria na Katiba ya nchi yetu,” alisema.
Pia, alielekeza kurekebishwa kwa sharti linalotaka kufungiwa kwa nyumba ya ibada endapo atakosea kiongozi, akisisitiza kuwa, anayekosea ndiye aadhibiwe bila kuathiri waumini kufanya ibada.
“Akikosea Sheikh, usiadhibiwe msikiti na akikosea Askofu, wasinyimwe waumini kufanya ibada, kwani ibada ni ushirika kati ya mwanadamu na Mungu wake, siyo yeye na askofu au sheikh,” alisema.
Waziri Mkuu aliambatana na Mawaziri na Naibu Mawaziri kutoka Wizara za Mambo ya Ndani, Ujenzi, Mambo ya Nje, Ofisi ya Rais (Uwekezaji), Viwanda na Biashara, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) na Uchukuzi.
Pia, aliwataka vijana, Watanzania na makundi mbalimbali, kuanzia ngazi ya familia, dini kutokubali vurugu zilizotokea Oktoba 29, mwaka huu zisitokee tena.
“Tumeona madhara na madhara mengi hayana fidia. Tuiache kabisa njia ile,”alibainisha Dk. Mwigulu.
“Tukio lile lilikuwa na madhara ya upotevu wa maisha, wapo ambao hawakuhusika na hawakuwa na hatia. Katika imani yangu, damu ya mtu asiye na hatia kumwagika siyo baraka.
“Wanaoshabikia wengi hawako ndani ya nchi yetu. Hawako wao wala familia zao, mimi niwambie waliowatuma na waliotumwa, wale wanaomezea mate rasilimali za Watanzania rasilimali zitalindwa kwa gharama isiyo hesabika. Zitalindwa kwa gharama yote. Watanzania amkeni.
“Mnajua wangapi katika vurugu zilipokuwa zikiendelea walikuwa na silaha? Mnajua polisi waliodhurika ni wangapi? Wangapi hata Kiswahili walikuwa hawaongei? Na Mnachochewa mwende tena? Kataeni kuna kitu mnachezewa. Hiyo siyo siasa,”alisema.
WAZIRI TAMISEMI
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe, alisema sh. bilioni 12.5, zitatumika kukarabati miundombinu ya BRT iliyoathiriwa Oktoba 29, mwaka huu.




