Na ZIANA BAKARI
BAADHI ya wadau wakiwemo wasomi na wanasiasa wakongwe, wameipongeza kasi iliyoanzwa na Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba na baadhi ya mawaziri kusimamia vyema majukumu yao.
Miongoni mwa majukumu hayo ni utekelezaji wa ahadi yale ambayo Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ndani ya siku 100.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na UHURU, baadhi ya wasomi na wanasiasa hao, walisema Dk. Mwigulu na baadhi ya mawaziri, wameanza vizuri, wanapaswa kupongezwa kwa uwajibikaji tangu walipoapishwa na Rais Dk. Samia.
DK. DANINGA
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA), Dk. Philip Daninga, aliwapongeza viongozi hao, kuanza kuchukua hatua dhidi ya watumishi wa umma wasiofanya kazi kwa uadilifu.
Dk. Daninga, alisema ni jambo zuri kwa kuwa, linatoa taswira ya namna ya viongozi wanavyopaswa kuwajibika kwa wananchi.
Kwa mujibu wa Dk. Daninga, watumishi wa umma, wanatakiwa kusoma alama za nyakati, zikiwemo za kufanya kazi kwa bidii, uadilifu kwa lengo la kuwaletea wananchi maendeleo.
“Tunapenda kuona ziara hizi zinazofanywa na baadhi ya mawaziri za kushtukiza, zinaendelea kwa sababu, zitasaidia sehemu kubwa ya watumishi wa umma kuwajibika ipasavyo kwa wananchi.
“Niwaombe sana wananchi, kuwa na imani na serikali kwa sababu, maendeleo yote yanayoonekana nchini, yanatokana na jitihada kubwa zinazofanywa na serikali, hivyo tuipende na tushirikiane na viongozi wetu,”alisema.
DK. LYANGA
Naye Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Dk. Timothy Lyanga, alisema serikali iliyoingia madarakani, inasimamia vyema majukumu yake kwa vitendo, jambo ambalo ni moja ya kasi za utekelezaji za ndani ya siku 100 alizotangaza Rais Dk. Samia.
Alisema ana imani Baraza la Mawaziri, litatatua changamoto za wananchi na kuwasimamia vyema watumishi wa umma, kuwajibika ipasavyo.
Dk. Lyanga alisema kuwa, wanatarajia matokeo chanya ambayo yatakuwa chachu ya kutatua changamoto za wananchi na kusimamia vyema miundombinu.
“Niwaombe sana watumishi wa umma, wasifanye kazi kwa mazoea, wajikite zaidi katika kuwaletea wananchi maendeleo jambo ambalo ni muhimu na linapaswa kupewa kipaumbele,”alisema.
CHILIGATI
Mwanasiasa mkongwe nchini, Kapteni Mstaafu John Chiligati, aliwasihi viongozi waliopewa majukumu na Rais Dk. Samia, kuyasimamia vyema muda wote.
Kwa mujibu wa Chiligati, watumishi wa umma, wanapaswa kufanya kazi kwa weledi, uamini na uadilifu wanapokuwa katika kazi zao, hususan za kuwahudumia wananchi.
Novemba 15, mwaka huu, Waziri Mkuu, Dk. Nchemba, alipokuwa mkoani Dodoma, alifanya ziara ya kushtukiza katika Hospitali ya Benjamin Mkapa ya Mkoa wa Dodoma, ambapo aliagiza hospitali zote nchini, zihakikishe wajawazito wanahudumiwa haraka kuokoa maisha ya mama na mtoto.
Pia, aliiagiza Wizara ya Afya, Bohari ya Dawa (MSD) na hospitali zote, ziweke vipaumbele vya kuwa na dawa, kulingana na mahitaji ya eneo husika.
“Haipendezi mwananchi kufika hospitali na kuwapatia vipimo vyote kisha anaambiwa dawa akanunue kwingine, kama duka binafsi linaweza kupata dawa hizo, inawezekanaje hospitali za serikali hazipati, naagiza hospitali zote ziwe na dawa,”alisema Waziri Mkuu.
Aidha, Novemba 21 mwaka huu, Waziri Mkuu alikagua mradi wa kituo cha ukaguzi cha pamoja kilichopo Muhalala mkoani Singida, baadae, aliagiza Jeshi la Polisi na Uhamiaji, kuhakikisha wanamkamata na kuzuia hati ya kusafiria ya mkandarasi anayejenga mradi huo uliopaswa kukamilika mwaka 2018.
“Mkandarasi huyu alitangazwa amefilisika na hawezi kuendelea na mradi na alielekezwa ailipe fidia Tanzania kwasababu ameicheleweshea mradi, naelekeza, Kamishna wa Uhamiaji, kamata hati yake ya kusafiria, asitoke nje ya nchi hadi jambo hili liishe, hii ni hujuma ya waziwazi anaifanyia nchi yetu, Jeshi la Polisi mtafuteni mkandarasi huyu popote alipo,” alisisitiza Dk. Mwigulu.
Katika hatua nyingine, Novemba 23 mwaka huu, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, alipokuwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Morogoro ya ukaguzi wa miradi ya dharura (CERC), aliagiza kusimamishwa kazi watumishi wa Wakala wa Barabara wa Taifa (TANROADS), waliohusika na uzembe wa kutoshughulikia tatizo la mizani ya Mikese mkoani humo.
“Hii haiwezi kukubalika, wananchi wanateseka kwa kukaa njiani muda mrefu, biashara zinadumaa. Sitaki kumuonea mtu nataka majibu nani amesababisha hii na kuchukua hatua kwa haraka,”alisema Ulega.
Novemba 18, mwaka huu Rais Dk. Samia alipokuwa akiwaapisha mawaziri na naibu mawaziri Ikulu, Chamwino mkoani Dodoma, alisema hatasita kuwabadilisha atakapobaini wameshindwa kuwajibika ipasavyo kuwaletea wananchi maendeleo.




