Na ZIANA BAKARI
“MPIRA wa miguu ulikuwa katika damu, niliupenda mwenyewe kucheza tangu nilipokuwa mdogo, sikukubali kukatishwa tamaa na mtu yeyote yule nilihakikisha nafikia malengo niliyojiwekea.
“Namshukuru Mwenyezi Mungu hadi kufika hapa nilipo, kwa sababu kila jambo linatokana na baraka zake, jambo la msingi nililozingatia katika maisha yangu ni kuhakikisha nasimamia kipaji changu kufikia pale nilipopanga kufikia,” hiyo ni kauli ya Salum Athuman.
Hayo ni maneno ya Salum Athuman Salum, anayefahamika kwa mashabiki zake kwa jina la ‘Stopper’ ni beki kisiki wa timu ya KMC FC, ambaye aliweka wazi safari yake ya soka imejaa juhudi na matumani makubwa ya siku moja kuichezea timu kubwa nje ya nchi.
Inafahamika wazi kuwa, sekta ya michezo imezidi kupata mafanikio makubwa yanayochangiwa kwa kiasi kikubwa na juhudi zinazotekelezwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Rais Samia amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha anaisaidia sekta ya michezo kupiga hatua zaidi ili vijana wapate ajira kupitia michezo na kukuza vipato vyao. Hayo yote yanatokana na kuwepo Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) yenye kuiongoza serikali kukuza michezo nchini.
Tanzania ni moja ya nchi iliyojaliwa vipaji vya michezo mbalimbali ambapo vijana wamekuwa wakijiajiri kupitia sekta hiyo na kutiangaza vizuri nchi nje ya mipaka yetu.
Miongoni mwa michezo iliyopiga hatua ni mchezo wa mpira wa miguu ambao umekuwa na mashabiki wengi hapa nchini.
Tayari vijana wengi wamekuwa wakionyesha juhudi ya kupambana na kufikia malengo waliojiwekea licha ya changamoto mbalimbali zinazowakabili.
Katika jitihada za kuangazia vipaji vya soka nchini, gazeti hili hivi karibuni limepata nafasi ya kufanya mahojiano maalumu na beki huyo anayechezea namba nne na tano katika timu ya Manispaa ya Kinondoni maarufu KMC inayoshiriki michuano ya Ligi Kuu Tanzania B ara msimu huu.
Salum alisema amezaliwa jijini Dar es Salaam ni mtoto wa kwanza katika familia ya watoto wawili.
Kwa mujibu wa Salum, babu yake na baba zake wadogo waliwahi kuwa wachezaji, japokuwa hawakupata bahati ya kucheza katika ngazi ya kubwa.
SAFARI YA SOKA
Akizungumza katika mahojiano maalumu, beki huyo alisema kwamba safari yake ya soka ilianza rasmi katika kikosi cha Simba B na baadae alijiunga na timu ya Fountain Gate.
“Baada ya kujiunga na timu ya Fountain Gate,nlitoa mchango mkubwa wa kuipandisha timu daraja, baadaye alichezea timu za Ndanda FC, JKT Tanzania, Mbeya Kwanza, KVZ ya Zanzibar na hatimaye alijiunga na KMC,”alisema.
Pia,mchezaji huyo alisema alianza kucheza soka tangu alipokuwa na umri mdogo, licha ya baadhi ya changamoto kumkuta.
“Nilianza soka nikiwa na miaka 10 tu, nilikuwa nikicheza mitaani na baadaye nilijiunga na timu ya shule, nilipambana na nilihakikisha nakisimamia kipaji changu licha ya changamoto mbalimbali ninayopitia.
“Ndoto yangu kubwa ni kuja kuwa mchezaji wa kulipwa, nilijiunga na timu ya vijana ya mkoa jijini Dar es Salaam, kabla ya kujiunga rasmi na klabu ya KMC,” alisema.
Beki huyo alisema anaendelea kupambana ili kuhakikisha anapata namba katika kikosi cha kwanza cha timu hiyo.
VIPAJI VYA SOKA NDANI YA FAMILIA
Beki huyo wa KMC alisema vipaji vya soka vilikuwapo katika ukoo wao, kwa sababu, babu yake na baba zake wadogo waliwahi kucheza mpira wa miguu.
“Namshukuru Mwenyezi Mungu nimejitahidi kusimamia kipaji changu, nitaendelea kukikuza na kufuata maelekezo yote ya m akocha wangu na viongozi wangu, nafashamu mafanikio siku zote hayaji bila ya kupambana,” alisema.
KUCHAGUA NAFASI YA BEKI
Akizungumzia kwa nini alichagua kucheza nafasi ya ulinzi, beki huyo alisema ana amini uwezo anao.
“Niliamini nina uwezo mkubwa wa kusoma mchezo, kuwa mtulivu na kusaidia kuongoza safu ya ulinzi, nafasi hii inanipa nafasi ya kuisaidia timu kwa namna ya kipekee.” alisema.
CHANGAMOTO ZA UWANJANI
Beki huyo alisema kuwa kazi ya uwanjani siyo rahisi, kwa sababu mara nyingi wanakutana na changamoto ya washambuliaji wenye kasi, nguvu na uzoefu mkubwa.
Kwa mujibu wa beki huyo, muda mwingine wanapata changamoto ya presha kutoka kwa mashabiki ambayo imekuwa na msukumo mkubwa.
“Mara nyingi tunakutana na washambuliaji wenye kasi, nguvu na uzoefu mkubwa. Pia muda mwingine presha kutoka kutoka kwa mashabikiinakuwa changamoto kwetu tunapokuwa uwanjani,”alisema.
MAISHA YAKE YA KMC
Beki huyo alisema kwamba, akiwa KMC amejifunza mambo mengi kupitia
benchi la ufundi na wachezaji wenzake.
Kwa mujibu wa Salum, alisema wachezaji wenzake na benchi la ufundi wamekuwa wanampa ushirikiano wa kutosha na kumpa nguvu ya kuendelea kupambana kusaka namba katika kikosi hicho.
“Najivunia kuwa sehemu ya timu hii. nimejifunza vitu vingi sana kutoka kwa benchi la ufundi, namnshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema hadi hivi sasa.
“Nilichojifunza katika maisha ni kumheshimu kila mtu, akiwa mdogo au mkubwa jambo la muhimu ni kuhakikisha unakuwa na heshima na kufanya kazi kwa ushirikiano na wenzako,” alisema.
ATAMANI KUCHEZA LIGI KUBWA BARANI AFRIKA
Beki huyo aliweka wazi kuwa, ndoto yake kubwa anatamani kucheza ligi moja wapo kubwa barani Afrika au hata ulaya.
“Kwa kweli natamani siku moja kuvaa jezi ya timu ya Taifa ‘Taifa Stars’,ili nitoe mchango wangu wa kupeperusha vizuri bendera ya Tanzania.” alisema.
Hata hivyo,mchezaji huyo alisema anapenda kucheza nje ya nchi ili kutengeneza maisha yake na kukuza uchumi kwa ujumla.
USHAURI KWA VIJANA
Kwa mujibu wa beki huyo, vijana wanaotamani kuwa wachezaji , aliwataka kuzingatia mafunzo ya makocha na kufanya mazoezi kwa nguvu zote.
“Viajna wanapaswa kujua kuwa soka linahitaji kujitoa, wapo wengi wenye vipaji lakini nidhamu inawakwamisha naamini ukijitambua, unaweza kufika mbali.” alisema.
Pia, aliwasihi mashabiki wa KMC kuendelea kumuunga mkono na kuendelea kumpa nguvu za kuendelea kusimamia kipaji chake.




