Na IRENE MWASOMOLA
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ameeleza namna alivyowasaidia wanasiasa waliokuwa wamekimbilia nje ya nchi na kusema kwamba, siasa siyo kuharibu nchi, kubezana na kutukanana, bali ni uungwana.
Pia, amesema kwa dhamira ya kujenga nchi, alianzisha upatanishi na vyama vya upinzani kwa kufanikisha waliokuwa nje, kurejea na kufutiwa kesi zilizokuwa zikiwakabili.
Akilihutubia taifa jijini Dar es Salaam, katika mkutano wake na wazee wa mkoa huo, Rais Dk. Samia alisema baada ya kuingia madarakani, alitoa fursa muhimu kwa vyama vya siasa, ikiwemo kufanya mikutano na shughuli za kisiasa baada ya kuzuiwa miaka saba.
“Siasa siyo kutukanana, siyo kubezana, siasa siyo kuharibu nchi. Wazee wetu wa zamani ukiwa na harakati hizo walikuwa wanasema huyu hajui siasa, siasa maana yake ni usalama na uungwana.
“Mwaka 2020 hadi 2023 nilifanya kazi kubwa ya kuzungumza nao nikanyoosha mkono wa rehema njooni Watanzania, njooni tukae tukazungumze yetu.
“Nikidhani nawanyooshea Watanzania mkono wa rehema na wataupokea watakuja tukae vizuri ni hawa hawa niliowakuta nje wana ‘suffer’ (wanahangaika) hawana hata shilingi, nikatoa kiposho changu nilichogawiwa cha safari nikawapa waendelee na maisha wakiwa nje,” alisema.
Aidha, Rais Dk. Samia alisema serikali haikuzuia chama chochote cha siasa kushiriki Uchaguzi Mkuu Oktoba 29, mwaka huu, ambapo chama ambacho hakikushiriki kilijiondoa baada ya kuona dalili za kushindwa na mipasuko waliyokuwa nayo.
ATOA NENO KWA VIONGOZI WA DINI
Aidha, Rais Dk. Samia aliwaomba viongozi wa dini kusimama na kutekeleza majukumu yao, kuhakikisha hawatumiki kuvuruga nchi.
Dk. Samia alisisitiza iwapo kuna jambo lolote, njia sahihi za kukaa na kufanya mazungumzo zipo ambazo ni kukaa na kujadiliana.
Alibainisha hakuna eneo baya la kumpata mwananchi kama ndani ya dini, kwani mtu anapolishwa maneno kupitia dini inabaki ndani ya moyo tofauti na siasa ambayo huingia akilini na baadaye kuondoka baada ya jambo zuri kuja.
“Viongozi wetu wa dini kaeni katika mstari wenu, dini zetu zote zinasema kila mamlaka imeletwa na Mungu iwe kuna mwanamke, mwanaume na sababu ya Mungu kuleta mamlaka hiyo hakuna anayeijua,” alisema.
Vilevile, Rais Samia alisema ubora wa dini uko mioyoni mwa waumini na kusisitiza nchi haitaendeshwa na madhehebu ya dini, kwani serikali haina dini.
Aliongeza hakuna kitabu cha dini kinachosema dini zitatumika kuvuruga nchi, ila ni utashi wa watu binafsi ambao hutumia vivuli vya dini.
“Msivae majoho ya dini kutengeneza utashi wenu binafsi kupitia vivuli vya dini niwaombe sana viongozi wa dini tusimame tusivuruge nchi yetu,” aliongeza.
Rais Dk. Samia alieleza serikali itaendelea kusimama na kuilinda nchi kwa nguvu zote.




