Na MWANDISHI WETU
VIONGOZI wa Klabu ya Simba, wametakiwa kujitathmini kuhakikisha wanainusuru timu hiyo ili ifanye vizuri katika michuano mbalimbali.
Uongozi wa Klabu ya Simba, juzi ulifanya Mkutano Mkuu wa Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na wajumbe mbalimbali.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wadau wa Simba, walisema uongozi unatakiwa kujitathmini kuhakikisha wanainusuru timu ili ifanye vizuri.
Mchezaji wa zamani wa Simba, Abdallah Kibadeni, alisema viongozi wa klabu hiyo wanatakiwa kujitathmini kuhakikisha wanainusuru timu yao.
Alisema ndani ya uongozi wa Simba kuna migogoro baina yao, hivyo wanachotakiwa ni kukaa pamoja na kuzungumza ili kujua chanzo cha matatizo na kuyapatia suluhusho kwa manufaa ya klabu kwa ujumla.
Alisisitiza hata kwa upande wake hakualikwa wala kushirikishwa kitu chochote kuhusu mkutano huo kitu ambacho siyo kizuri kwani wachezaji wakongwe wana mchango mkubwa ndani ya uongozi wa Simba na klabu kwa ujumla, hivyo wanatakiwa kushirikishwa vitu vinavyoendelea ili kutoa ushauri wao.
“Mimi mwenyewe nilishtushwa baada ya kupigiwa simu na watu waliokuwa wapo ndani ya mkutano kwani sikushirikishwa kwa kitu chochote japokuwa siyo kiongozi lakini nina mchango mkubwa ndani ya Simba.
“Sikwenda kwani sikualikwa na niliona viongozi waliopo inawezekana wanajiweza lakini wengi wamelalamika jinsi mwenyekiti alivyomaliza mkutano.
“Mimi ni mmoja wa watu nilioipa Simba mafanikio makubwa kipindi ninacheza na baadaye kocha, lakini bado nina mchango mkubwa kwa klabu kama wangekuwa wakiuhitaji.
“Watu hawataki kunitumia hivyo siwezi kuwalazimisha kwani kila mmoja anatambua uwezo wangu maana nimutumikia soka miaka 50 katika nyanja mbalimbali.
“Uongozi unatakiwa kujithmini kwani kuna tatizo ndani ya Simba, hakuna mtu anapenda kufungwa, watu wanalalamika wameshachoka kufungwa kila siku.
“Viongozi wajitazame wanakosea wapi na kurekebisha kasoro zao kuhakikisha timu inafanya vizuri kama ilivyokuwa awali, wachezaji wa zamani wanatakiwa kuhusishwa ili wasaidiwe kwa mambo mbalimbali,” alisema Kibadeni.
Kwa upande wa mchezaji wa zamani wa Simba, Zamoyoni Mogella, alisema siku zote kama kuna uongozi una matatizo hata timu haiwezi kufanya vizuri kwa namna yoyote.
Alisema hata timu ilipokwenda nchini Mali kwa mechi ya pili ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL), dhidi ya Stade Malien, hakuna kiongozi mkubwa aliofuatana nao kwa ajili ya kuwapa sapoti, viongozi wote walijikitika katika mkutano kitu ambacho siyo sahihi.
Alisisitiza kwamba timu ilipata matokeo mabaya kwani chanzo kilianzia kwa viongozi kushindwa kwenda kuipa sapoti ya kutosha timu ilipokuwa ugenini.
“Shida ipo kwa uongozi unatakiwa kujifanyia tathmini kuhakikisha Simba inarudi katika makali yake kama zamani.
“Viongozi wanatakiwa kukaa pamoja na kuzunguza ikiwemo kujitafakari, watapata ufumbuzi na tutaanza kuiona timu ikifanya vizuri katika michuano mbalimbali,” alisema Mogella.
Naye Mwenyekiti wa Simba, Murtaza Mangungu alisema aliahirisha mkutano baada ya kumaliza ajenda zote na hakukuwa na hoja ya ziada.
“Niliongoza mkutano na baadaye niliuahirisha kutokana na ajenda zote kumalizika na hakukuwa na hoja ndiyo nilipoamua kuuahirisha,” alisema Mangungu.




