Na MWANDISHI WETU
BAADA ya kupoteza mchezo wa pili dhidi ya Stade Malien, Meneja Mkuu wa Simba, Dimitar Pantev amesema sababu kubwa ya kushindwa kupata matokeo ni wachezaji wake kucheza chini ya kiwango.
Simba, juzi ilifungwa mabao 2-1 dhidi ya Stade Malien, katika mchezo wa pili wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL), uliofanyika Uwanja wa 26 du Mars, Bamako nchini Mali.
Huo unakuwa mchezo wa pili kwa Simba kupoteza kufuatia kukubali kufungwa bao 1-0 dhidi ya Petro Atletico ya Angola, mechi ya kwanza iliyofanyika Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Kufuatia matokeo hayo, katika msimamo wa kundi D, Simba inaburuza mkia baada ya kupoteza mechi mbili za mwanzao, Petro Atletico ipo kileleni kwa pointi nne sawa na Stade Malien zikitofautiana mabao ya kufunga na kufungwa huku Esparace ikishika nafasi ya tatu ikiwa na pointi mbili.
Akizungumza mara baada ya mchezo huo kumalizika juzi, Meneja Pantev alisema walishindwa kupata matokeo ugenini kutokana na wachezaji wake kucheza chini ya kiwango.
Pia walifanya mazoezi bila ya wachezaji waliotitwa katika timu ya Taifa Stars kitu ambacho kilisababisha kushindwa kupata ushindi.
Alisema japokuwa walicheza chini ya kiwango, wachezaji wake walijitahisi kupambana kupata ushindi lakini bahati haikuwa upande wao.
Alisisitiza kuwa hataki kujitetea, hivyo anakubali mashabiki kuchukia kwa sababu wana matarajio makubwa kwa muda mfupi.
Alisema ameshayaona baadhi ya makosa ambayo waliyafanya na kwamba anakwenda kuyatafutia ufumbuzi ikiwemo uboreshaji wa kikosi ili kuja kivingine na kuwapa raha mashabiki.
“Tulicheza chini ya kiwango katika mechi yetu ya ugenini awali tulifanya mazoezi bila ya wachezaji wa Taifa Stars kitu ambacho kilitugharimu.
“Nimeyaona baadhi ya makosa ambayo tuliyafanya ugenini, nitakwnda kuyafanyia kazi ikiwemo uboreshaji wa kikosi ili kuja kivingine na kuwapa raha mashabiki wetu,” alisema Pantev.
Aliongeza kwa kipindi cha miezi miwili aliyokaa klabuni hapo haitoshi kutimiza kile alichotakiwa kukifanya, lakini ni ukweli kwamba kwa timu kubwa kama hakuna muda wa kushuburi.
Alisema amekasirika kushindwa kuwafunga Stade Malien kwa sababu timu yake ni bora kuliko wapinzani wao.
Pantev alisema Simba ilitengeneza nafasi nyingi za kufunga lakini wachezaji wake walishindwa kuzitumia kupachika mabao wavuni.
Naye kiungo mshambuliaji wa Simba, Neo Maema alikiri kuumizwa na matokeo hayo kwani kama wachezaji walijiangusha wenyewe pamoja na mashabiki kuwaunga mkono kwa kiasi kikubwa.
Maema alisisitiza kuwa matokeo ya kupoteza mechi mbili mfululizo kwa timu kubwa kama Simba yanaumiza, lakini hawana cha kujitetea zaidi ya kurudi upya na kuanza kukusanya pointi katika mechi zilizobakia.
“Matokeo yanaumiza kwa kiasi kikubwa japokuwa tunaendelea kupewa sapoti na mashabiki wetu, hatuna cha kujitetea zaidi tunatakiwa kujipanga upya ili kuanza kukusanya pointi katika mechi zilizobakia,” alisema.




