Na Mwandishi Wetu
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan amekutana na Kaimu Balozi wa Marekani nchini, Andrew Lentz, pamoja na mambo mengine wamejadili ushirikiano wenye faida kwa nchi zote mbili.
Mkutano huo kati ya Rais Dk. Samia na Kaimu Balozi Lentz ulifanyika Ikulu, Chamwino jijini Dodoma huku wakiazimia kuendeleza ushirikiano wenye manufaa ya pamoja na kuendeleza mikataba ya ushirikiano baina ya mataifa hayo.
Kwa mujibu wa taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu, iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana, katika mazungumzo hayo Balozi Lentz, ambaye aliambatana na Kamisaa wa Siasa na Masuala ya Uchumi wa ubalozi huo, alielezea dhamira ya Marekani katika kuendeleza uhusiano katika nyanja ya uchumi, siasa na usalama baina ya mataifa hayo mawili.
“Marekani imedhamiria siyo katika ushirikiano tegemezi wa misaada, bali wenye manufaa kwa mataifa yote mawili,“alifafanua Kaimu Balozi Lentz.
Sehemu ya taarifa hiyo ya Ikulu iliongeza, mkutano huo ulihusu majaliano yaliyojikita katika miradi ya kimkakati ya Marekani na Tanzania ambayo iko kwenye majadiliano.
MIRADI YA KIMKAKATI
Taarifa hiyo iliongeza kuwa, pande zote mbili zinatambua mchakato wa majadiliano wa miradi hiyo kati ya Marekani na Tanzania ukiwemo wa gesi asilia (LNG), mradi Tembo Nickel, ambayo yote iko katika hatua za mwisho za kusubiri utiaji saini.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya Ikulu, mradi wa tatu uliojadiliwa ni wa machimbo ya madini ya Graphite, uliopo Mahenge, mkoani Morogoro ambao bado unafanyiwa kazi.
RAIS DK. SAMIA
Kwa upande wake, Rais Dk. Samia alipongeza dhamira ya Marekani na kuahidi kwamba Tanzania iko tayari kuhakikisha hatua zilizosalia katika miradi hiyo zinakamilishwa.
“Kama nchi isiyofungamana na upande wowote, iko wazi, tayari na imedhamiria kushirikiana na wadau wote ambao wanaheshimu uhuru wetu na maono yetu kwa ustawi wetu,” alisema Rais Dk. Samia.
“Miradi hii ya kimkakati ina umuhimu mkubwa kwa taifa na tumedhamiria kuikamilisha kwa ajili ya kutoa ajira, uwekezaji na ustawi endelevu wa watu wetu,”alisisitiza Rais Samia.
Rais Dk. Samia alitaja kampuni 400 za Marekani zinazofanya kazi nchini kwamba ni uthibitisho wa umadhubuti, uwazi na ushirikiano wa kiuchumi wa muda mrefu na Marekani.
Mbali na uwekezaji, mazungumzo hayo yaligusia kwa kina masuala ya ushirikiano likiwemo la utulivu wa kisiasa, usalama wa kikanda, mageuzi ya kiuchumi, ukuaji wa sekta binafsi, sekta ya afya na uhusiano kati ya raia wa mataifa hayo mawili.
KAIMU BALOZI LENTZ
Kaimu Balozi Lentz, alimpongeza Rais Dk. Samia kwa maono na mipango yake madhubuti kupitia Dira ya ya Taifa ya Maendeleo 2050, na kusisitiza kwamba serikali ya Marekani iko tayari kusaidia utekelezaji wake huku akielezea kuguswa na Falsafa ya 4R katika uongozi.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya Ikulu, pande zote mbili zilikubaliana kuimarisha mawasiliano ya mara kwa mara na kuchukua hatua kwa wakati katika utekelezaji wa makubaliano kwa lengo la kuondoa vikwazo katika ushirikiano baina ya mataifa hayo.
THAMANI YA MIRADI
Mradi wa LNG unakadiriwa kuwa thamani ya Dola za Marekani bilioni 42, ambao ukikamilika utazalisha maelfu ya ajira, kukuza pato la taifa na kuifanya Tanzania kuwa msafirishaji mkubwa wa LNG duniani.
Tembo Nickel ni mradi wenye thamani ya Dola milioni 942 million, uliopo Ngara, Kagera unahusisha madini muhimu ya utengenezaji wa betri za magari ya umeme, utakaochochea ukuaji wa viwanda, kusaidia usambazaji wa nishati safi duniani na kuongeza mapato ya mauzo ya nje.
Mradi wa Mahenge Graphite wenye thamani ya Dola za Marekani milioni 300, ni moja ya miradi mikubwa duniani utakuza uzalishaji wa betri, nishati jadidifu na kuiweka Tanzania katika nafasi ya kuwa kinara wa usambazaji wa madini hayo yanayotumika kutengeneza betri duniani.




