Na NASRA KITANA
IKIBAKI wiki moja kabla ya dirisha dogo la usajili katika Ligi Kuu Tanzania Bara kufunguliwa, klabu ya Yanga inakaribia kunasa saini za washambuliaji Emmaniel Mwanengo na Laurindo Depu.
Mwamengo raia wa Tanzania anayekipiga TRA United na Muangola Depu kutoka Radomiak Radom ya Poland, wanatakiwa na Yanga kuboresha kikosi kwa michuano ya Ligi Kuu Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL) msimu huu.
Kwa mujibu wa chanzo cha kuaminika, Yanga imepanga kuwanasa nyota hao na wengine huku ikilenga kuwatoa kwa mkopo baadhi ya nyota wake, kusalia na kikosi ambacho kitakuwa tishio.
UHURU ilipomtafuta Ofisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe, aligoma kuwazungumzia wachezaji hao huku akisema klabu tayari imeshaanza kufanyia kazi ripoti ya kocha wake, Pedro Goncalves.
Kamwe amesema viongozi wao tayari wapo mawindoni kutafuta wachezaji ambao mwalimu anawahitaji.
Amesema Pedro ataongeza wachache ili kuboresha timu katika nafasi ambazo ameona zina mapungufu kufanya vizuri katika mechi zinazokuja.
“Sisi tutafanya usajili mapema zaidi kukimbizana na muda, tunataka tukimsajili mchezaji acheze mechi inayofuata dhidi ya Al Ahly ya Misri, siyo kusubiri taratibu, sijui vibali, kama yupo anasajiliwa moja kwa moja anakwenda katika mazoezi,” amesema Kamwe.
Yanga inashika nafasi ya pili katika Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi 16 katika mechi sita, ikishinda mechi tano na kutoka sare moja.
Katika CAFCL, Yanga ipo nafasi ya pili katika kundi B ikiwa na pointi nne baada ya kushuka dimbani mara mbili, ikishinda mechi moja na kutoka sare moja.
Timu hiyo ipo sawa na kinara Al Ahly ya Misri zikitofautiana mabao ya kufunga na kufungwa, AS FAR Rabat ya Morocco na JS Kabylie ya Algeria zikifuatia kila moja ikiwa na pointi moja.
Yanga ilianza kwa ushindi wa bao 1-0 dhidi ya AS FAR nyumbani kabla ya kutoka suluhu dhidi ya JS Kabylie ugenini.




