Na IRENE MWASOMOLA
WATAALAMU wa maji nchini, wameshauri mbinu nane kuondoa changamoto ya uhaba wa maji inayolikabili jiji la Dar es Salaam kila mara.
Wameshauri ijengwe miundombinu ya uvunaji maji ya mvua katika makazi ya wananchi, kianzishwe chanzo kutoka Mto Rufiji, matumizi ya maji ya bahari yatakayoambatana na mitambo ya kisasa ya kupunguza chumvi, kuongeza ujenzi wa mabwawa na kuchimba visima virefu.
Pia, serikali ijenge mabwawa madogo ya kuvuna maji ya mvua, Mto Msimbazi uwe chanzo kimojawapo cha maji na serikali kuanzisha mkakati kukabiliana na upotevu wa maji.
Mbinu hizo zimetolewa zikiwa zimepita siku tano tangu Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA), kutangaza kuna uhaba wa maji katika baadhi ya maeneo kutokana na kina cha Mto Ruvu kushuka.
Akizungumza na UHURU Dar es Salaam, Dk. Livingstone Swilla ambaye ni mhandisi wa mabwawa katika Chuo cha Maji (WI), alisema serikali inaweza kuwa na vyanzo vikubwa zaidi kwa kutumia Mto Rufiji ambao una maji mengi.
“Suluhisho la kudumu tunaloweza kulifanya ni kuwa na vyanzo vikubwa zaidi mfano mto Rufiji, mto Pangani na Wami.
“Tungekuwa na mabwawa madogo kipindi cha mvua, yawe yanadaka maji ya kutumika kwa shughuli ndogo ndogo, badala ya kutumia mabwawa makubwa au mito,” alisema.
Pia Dk. Swilla alisema wameshafanya utafiti na kubaini mto Msimbazi kunaweza kujengwa mabwawa madogo ambayo yatasaidia kupunguza uhaba wa maji.
Alibainisha kuna haja serikali kuja na mkakati maalumu wa kukabiliana na upotevu wa maji, ikiwemo kumwajibisha meneja yeyote anayekumbwa na shida ya ya maji katika eneo lake huku hali hiyo ikijirudia mara kwa mara.
Akizungumzia uvunaji wa maji ya mvua nyumbani, Meneja wa Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu WI, Dk. Josephine Gobry, alisema kuna teknolojia nyingi zinaweza kutumika kuvuna maji hayo na kuhifadhi katika matanki.
Alisema maji hayo yatasaidia kupunguza changamoto ya kupatikana huduma hiyo, kwani matumizi katika Jiji la Dar es Salaam yameongezeka, huku chanzo kimebaki kimoja cha mto Ruvu.
Dk. Gobry aliwasisitiza wananchi kuendelea kutunza na kulinda vyanzo na rasilimali za maji na kuwashauri wanaofanya shughuli za umwagiliaji, kutumia visima na kuacha kuchepusha maji ya mto Ruvu.
Kwa upande wake mtaalamu wa maji chuoni hapo, Dk. Clarance Kisiki, alisema Dar es Salaam ina kiasi kikubwa cha maji chini ya ardhi, lakini wananchi hawana elimu ya kutosha kuhusu uvunaji wa maji ya mvua.
Dk. Clarance aliishauri serikali kuandaa sera maalumu inayomtaka mwananchi anayepewa kibali cha ujenzi, nyumba yake iwe na miundombinu ya kuvuna maji ya mvua.
Alisema kila mwanachi akifanya hivyo itasaidia kukabiliana na changamoto za ukosefu wa maji.
Hata hivyo, Dk. Clarance alisema serikali inapaswa kuendelea kuwafuatilia wananchi wanaolima karibu na kingo za mito, kwani ni moja ya sababu ya uharibifu wa vyanzo vya maji.
Naye, Mkuu wa Idara wa Uhandisi wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira (WI), Dk. Eunice Makungu, alisema uchimbaji visima utasaidia kukabiliana na changamoto.
TAARIFA KUTOKA DAWASA
Taarifa iliyotolewa na DAWASA Desemba 6, mwaka huu, iliwataarifu wananchi wanaohudumiwa na mtambo wa kuzalisha maji Ruvu Chini, kuna upungufu wa maji uliosababishwa na kushuka kina cha maji cha Mto Ruvu.
“DAWASA inawataarifu wateja wanaohudumiwa na mtambo wa kuzalisha maji Ruvu chini kuanzia Bagamoyo, Tegeta, Boko, Mbezi Beach, Mwenge, Kinondoni, Mwananyamala, Masaki hadi Ilala.
“Kumekuwa na upungufu wa huduma ya maji kutokana na uzalishaji wa maji kushuka zaidi ya kiwango cha kawaida kufuatia kina cha Mto Ruvu kushuka na kuchelewa mvua,” iliongeza taarifa hiyo.




