Na AMINA KASHEBA
BONDIA wa ngumi za kulipwa, Emmanuel Mwaykembe amehaidi kutoa zawadi ya sikukuu ya Krisimasi katika pambano lake la Punch To Punch’ litakalofanyika Jumapili ya wiki hii.
Mwakyembe atapanda ulingoni kuzichapa na Tionge Chingeni kutoka Malawi katika pambano lisilo la ubingwa raundi nane, uzito wa kati litakalofanyika Ukumbi wa The Sea View Dome Banguel ulipo Kawe jijini Dar es Salaam.
Akizungumza Dar es Salaam, jana,bondia huyo alisema hivi sasa anafanya mazoezi mepesi huku akisubiri kupima uzito, keshokutwa katika Viwanja vya Las Vega Mabibo.
“Niko fiti kabisa nahitaji kutoa zawadi ya sikukuu ya Krisimasi kwa Watanzania wote na mashabiki zangu kwa ujumla,” alisema.
Mwakyembe aliongeza kuwa Watanzania wanapaswa kufurahia mafanikio ya mchezo wa ngumi na yeye atawapa.
“Hivi sasa Tanzania inafanya vizuri katika michezo mbalimbali ndiyo maana sisi mabondia tunapambana kuongeza bidii katika mazoezi, kuwapiga wapinzani wetu kutoka nje ya nchi kama kwangu nipo fiti na pambano langu kumchakaza Mmalawi,” alisema Mwakyembe.
Promota wa pambano hilo, Latifa Jabiri alisema mpinzani wa bondia Mwakyembe, ameshafika Tanzania anasubiri siku ya kupima uzito.
“Kila kitu kinaenda vizuri kutakuwa na mapambano makali nina imani wadau wa masumbwi watafurahi kwa sababu kila bondia atayepanda ulingoni ataonyesha mchezo nzuri na kutoa burudani ya kutosha,” alisema.
Promota huyo alisema kutakuwa na mapambano 15 ambayo wadau wa masumbwi watashuhudia vijana wakipimana ubavu.




