CAIRO, Misri
KIPA wa timu ya Taifa ya Nigeria, Stanley Nwabali ameshusha presha baada ya benchi la ufundi baada ya kujiunga na timu hiyo nchini Misri.
Nigeria imeweka kambi yake nchini humo kujiandaa na michuano ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2025) inayotarajiwa kufanyika nchini Morocco kuanzia Desemba 21, mwaka huu.
Timu hiyo imepangwa kundi C ikiwa na timu za Tunisia, Uganda na Tanzania huku mechi zote za makundi zikipangwa kuchezwa huko Fes.
Ujio wa Nwabali umeongeza mzuka katika kitengo cha makipa wa Nigeria ambapo mlinda mlango huyo ni chaguo la kwanza ndani ya kikosi hicho.
Nwabali aliwasili na kuondoa wasiwasi wa hivi karibuni, kufuatia kukutwa na tatizo la kifundo cha mguu, pia jeraha la mkono ambalo likiripotiwa kuhitaji kufanyiwa upasuaji.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 29, hajacheza ndani ya kikosi cha timu ya Chippa United tangu mchezo wa Nigeria dhidi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Nigeria itaingia katika AFCON 2025 ikiwa katika nafasi ya nne kwa ubora wa soka Barani Afrika.
Pia, timu hiyo inashika nafasi ya 38 ya viwango vya ubora duniani kote.
Nigeria imewahi kutwaa taji la AFCON, mwaka 1980, 1994 na 2013.
Imewahi kushika nafasi ya pili ya michuano hiyo ya AFCON mara 5 na imewahi kucheza fainali za Kombe la Dunia mara sita.
Timu hiyo imeelezwa kuwa ina kikosi chenye thamani zaidi ya Euro milioni 280.
Kikosi hicho kina jumuisha nyota kama Victor Osimhen, Ademola Lookman, Alex Iwobi, Calvin Bassey na Wilfred Ndidi.
Wakati huo huo, Nigeria leo itacheza mechi wa kirafiki dhidi ya Misri utakaopigwa Uwanja wa Kimataifa wa Cairo nchini Misri.
Misri katika michuano ya AFCON 2025 imepangwa kundi B ikiwa na timu za Zimbabwe, Afrika Kusini na Angola.




